Storm FM
Storm FM
22 August 2025, 11:42 am

Usalama ndiyo tunu ya kwanza katika tunu sita zinazoongoza mgodi wa GGML ambazo zinatajwa kuchochea uzalishaji pamoja na kutoa mwongozo kwa wafanyakazi wa GGML.
Na: Ester Mabula
Kampuni ya Geita Gold Minning Limited (GGML) imeendeleza kuiishi tunu yao ya kwanza ya USALAMA pamoja na kuinufaisha Jamii inayozunguka mgodi huo kupitia ufadhili wa programu ya mafunzo ya usalama barabarani kwa maafisa usafirishaji 932 wa pikipiki za magurudumu matatu maarufu bajaji na pikipiki maarufu bodaboda ili kusaidia kupunguza ajali za barabarani wilayani Geita.
Mafunzo hayo yaliyopewa kaulimbiu isemayo “Uendeshaji Salama Barabarani Unaanza na Wewe” yamezinduliwa jana Agosti 21, 2025 kwa kuhusisha mafunzo ya awamu ya kwanza kwa washiriki 491 ambao ni maafisa usafirishaji kutoka halmashauri ya manispaa ya Geita.

Mwakilishi wa Meneja Mwandamizi wa Mahusiano GGML, Elibariki Jambau amesema mbali na maofisa usafirishaji, elimu hiyo pia itafikishwa kwenye shule ambazo zitapatiwa mafunzo ya usalama barabarani.
Mkuu wa Polisi wilaya ya Geita OCD Renatus Katembo amewaasa maafisa usafirishaji kuzingatia elimu hiyo kwa umakini ili iweze kuleta matokeo chanya yaliyokusudiwa

Mwenyekiti wa umoja wa bodaboda mkoa wa Geita, Fred Fidel pamoja na mwenyekiti wa umoja wa madereva bajaji mkoa wa Geita Mussa Kisoke wameishukuru GGML kwa program hiyo na kueleza kuwa itasaidia kuongeza umakini na uzingatiaji wa sheria za usalama barabarani

Akizungumza kwa niaba ya madereva wengine Raban Emmanuel ametoa shukrani kwa GGML kutoa elimu pamoja na viaksi mwanga (reflector) huku akiiomba serikali kuboresha miundombinu ya barabara kwani pia ni kikwazo kwa baadhi ya maeneo