

3 April 2025, 4:40 pm
Kamishna wa Polisi (CP) Faustine Shilogile, Kamishna wa Polisi Jamii leo April 03, 2025 amefika ofisi ya mkuu wa mkoa wa Geita kwa ziara ya kikazi na baada ya kupokelewa April 02 na Kamanda wa Polisi mkoani Geita (SACP) Safia Jongo.
Na: Ester Mabula:
Akiwa mkoani Geita kesho April 04, 2025 atazindua programu maalumu ya Polisi Jamii (Community Policing Outreach Program) iliyoandaliwa kwa ufadhili wa Mgodi wa Dhahabu wa Geita (GGML) ambayo imelenga kuwajengea na kuimarisha uelewa na uwajibikaji kwa Jamii katika miradi ya Polisi Jamii.
Program hiyo itatolewa kwa maafisa, wakaguzi na Askari wa Jeshi la Polisi, viongozi wa serikali, taasisi mbalimbali pamoja na wananchi ili kuhakikisha jamii inaendelea kushirikishwa na kushirikiana na Jeshi la Polisi kuimarisha ulinzi na usalama.
Kamishna (CP) Faustine ameeleza kuwa kwa sasa Geita imepiga hatua kwa kuendelea kuimarisha ulinzi sambamba na kupungua kwa matukio ya uhalifu na kwamba wapo mkoani Geita ili kuongeza mikakati zaidi ya kukabiliana na uhalifu.
Katika hatua nyingine ameupongeza mgodi wa GGML kuendelea kujitoa na kunufaisha Jamii inayouzunguka kwani ni moja ya nguzo muhimu katika kuimarisha ulinzi na usalama
Kamanda wa Polisi mkoa wa Geita (SACP) Safia Jongo amesema mkoa wa Geita umepokea ugeni kwa mikono miwili na kueleza kuwa mpango huo utaleta matokeo chanya zaidi.
AIdha Kamanda Jongo ametoa rai kwa wananchi kuendelea kutoa taarifa juu ya matukio ya uhalifu kwani suala la usalama ni la kila mtu.
Katibu Tawala mkoa wa Geita Mohamed Gombati amesema ujio wa viongozi hao wa Jeshi la polisi utasaidia kujenga uelewa wa pamoja kwa wananchi na kupunguza vitendo vya Uhalifu kupitia elimu.