Storm FM

Walimu shule ya sekondari ya wavulana ya Geita wapongezwa

18 February 2026, 12:56 pm

Mgeni rasmi, diwani wa kata ya Kalangalala, Reuben Sagayika akizungumza katika hafla ya pongezi. Picha na Ester Mabula

Jumla ya wanafunzi 65 waliohitimu kidato cha nne katika shule ya sekondari ya wavulana ya Geita walipata ufaulu wa daraja la kwanza (division one).

Na: Ester Mabula

Walimu wa shule ya sekondari ya wavulana ya Geita (GESECO) wamepewa tuzo kufuatia ufaulu mzuri  wa daraja la kwanza (division 1) kwa  wanafunzi  65 wa kidato cha nne waliohitimu mwaka 2025.

Hafla ya pongezi imefanyika Februari 17, 2026 shuleni hapo na kuhudhuriwa na wanafunzi, walimu, wazazi pamoja na viongozi wa taasisi mbalimbali ambapo zawadi mbalimbali zimetolewa ikiwemo pikipiki pamoja na fedha kwa viwango tofauti tofauti.

Awali akisoma risala mbele ya mgeni rasmi, Makamu mkuu wa shule Mwl. Venance Mushi amesema shule hiyo inakabiliwa na uchakavu wa miundombinu sambamba na ukosefu wa uzio hali inayopelekea usumbufu kwa wanafunzi.

Sauti ya kaimu mkuu wa shule mwl. Venance Mushi
Kaimu mkuu wa shule, Mwalimu Venance Mushi akisoma risala mbele ya mgeni rasmi. Picha na Ester Mabula

Mgeni rasmi, Diwani wa kata ya kalangalala Reuben Sagayika  kwa niaba ya Mstahiki meya wa manispaa ya Geita amewapongeza walimu kwa kazi kubwa na nzuri huku akiwasilisha zawadi kutoka halmashauri ya manispaa ya Geita kwa walimu  na wanafunzi waliofanya vizuri.

Sauti ya mgeni rasmi, Diwani wa kata ya Kalangalala

Kuhusu changamoto ya miundombinu, Mgeni rasmi ameahidi kutoa kiasi cha shilingi milioni 2 huku akiahidi kukusanya fedha na vitendea kazi kutoka kwa wadu ili kukarabati uzio wa shule hiyo.

Sauti ya mgeni rasmi, Diwani wa kata ya Kalangalala
Mwl. Venance Mushi akikabidhiwa pikipiki na mgeni rasmi, miongoni mwa pikipiki tatu zilizotolewa kwa walimu watatu waliofanya vizuri zaidi. Picha na Ester Mabula

Katika hatua nyingine ofisi ya mbunge Jimbo la Geita mjini imetoa kiasi cha shilingi laki 5 kwa mkuu wa shule pamoja na shilingi laki 3 kila mmoja kwa walimu wa masomo yaliyofanya vizuri ambayo ilikabidhiwa na Katibu wa Mbunge Rizick Marko.

Sauti ya katibu wa Mbunge, Rizicki Marko
Sehemu ya muonekano wa uzio ambao unaendelea kujengwa shuleni hapo. Picha na Ester Mabula

Awali akiwasilisha salamu za mkurugenzi wa Manispaa ya Geita, Afisa elimu taaluma sekondari Singo Jumaamesema ofisi ya mkurugenzi wa manispaa inatarajia kuandaa hafla kubwa ya kuwapongeza walimu wa shule za sekondari  waliofanya vizuri kwenye matokeo.

Sauti ya Afisa elimu taaluma sekondari, Singo Juma
Baadhi ya wanafunzi waliokuwa katika hafla ya kuwapongeza walimu wa kidato cha nne. Picha na Ester Mabula