Storm FM

Hati za kimila 838 zatolewa kwa wananchi Nyang’hwale

26 January 2026, 6:04 pm

Mkuu wa Wilaya ya Nyang’hwale Bi. Grace Kingalame akimkabidhi hati mkazi wa Ihushi. Picha na Mrisho Sadick

Ugawaji wa hati za kimila ni sehemu ya mkakati wa Serikali wa kuhakikisha wananchi wanakuwa na umiliki halali wa ardhi.

Na Mrisho Sadick:

Kuelekea siku 100 za uongozi wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, wakulima na wafugaji wa vijiji viwili katika Wilaya ya Nyang’hwale, mkoani Geita, wameishukuru Serikali kwa kutatua changamoto ya muda mrefu ya ukosefu wa maeneo ya malisho na kilimo.

Wananchi hao wamekabidhiwa maeneo ya ardhi pamoja na hati za kimila 838, hatua iliyowezekana baada ya Serikali kumega ekari 3,101 kutoka Msitu wa Hifadhi wa Miyenze kwa matumizi ya wananchi, Mkuu wa Wilaya ya Nyang’hwale, Bi. Grace Kingalame, ameongoza zoezi la ugawaji wa hati hizo ambapo kijiji cha Bujulamiyenze kimepata hati 541 huku kijiji cha Ihushi kikikabidhiwa hati 297.

Mkuu wa Wilaya ya Nyang’hwale Bi. Grace Kingalame akimkabidhi Mkurugenzi wa Halmashauri ya wilaya ya Nyang’hwale kitabu maalumu chenye majina ya wote waliopatiwa hati. Picha na Mrisho Sadick

Wanufaika wa hati hizo wameipongeza Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa utekelezaji wa haraka wa zoezi hilo, wakisema limefanyika kabla ya kutimia siku 100 za uongozi wake, jambo linaloonesha dhamira ya Serikali katika kusikiliza na kutatua kero za wananchi.

Wakazi wa Bujulamiyenze na Ihushi wakiwa kwenye hafla ya ugawaji wa hati za kimila. Picha Mrisho Sadick

Akizungumza katika zoezi hilo, Mkurugenzi wa Mipango ya Matumizi ya Ardhi, Usimamizi na Uratibu kutoka Timu ya Mipango ya Matumizi ya Ardhi, Bw. Jonas Masingija, amesema ugawaji wa hati za kimila ni sehemu ya mkakati wa Serikali wa kuhakikisha wananchi wanakuwa na umiliki halali wa ardhi ili kuepusha migogoro na kuchochea maendeleo ya kiuchumi.

Sauti ya Ripoti hii na Mrisho Sadick