Storm FM
Storm FM
7 October 2025, 4:48 am

Kampuni ya Geita Gold Mining Limited (GGML) imeadhimisha miaka 25 tangu kuanzishwa kwake kwa kuandaa mashindano ya gofu katika viwanja vya Lake Victoria Golf Club vilivyopo ndani ya eneo la mgodi mkoani Geita.
Na: Ester Mabula
Mashindano hayo ni miongoni mwa shughuli kadhaa zinazofanyika mwaka huu kuadhimisha miaka 25 ya GGML, zikiwa na lengo la kutafakari safari ya kampuni na mchango wa watu waliounda urithi huu, wakiwemo wafanyakazi, wanajamii, na Serikali.
Tukio hilo limehusisha wafanyakazi wa GGML na kampuni washirika mbalimbali, likilenga kuhamasisha afya, ushirikiano, na ustawi wa kijamii kupitia michezo.

Akizungumza kwa niaba ya uongozi, Afisa Mwandamizi wa Mawasiliano GGML, Rhoda Lugazia, amesema mchezo wa gofu ni sehemu ya kusherehekea mafanikio ya kampuni katika kipindi cha miaka 25 na unawakilisha maadili ya mshikamano na nidhamu kazini.

Washiriki walitoka katika vitengo mbalimbali vya kampuni, wakiwemo wahandisi, wataalamu wa mazingira, usalama kazini, na mawasiliano. Pia walihudhuria wageni kutoka taasisi za serikali na sekta binafsi, kama sehemu ya kuimarisha uhusiano wa kijamii.
Kupitia programu zake za uwajibikaji kwa jamii (CSR), GGML imeendelea kuunga mkono maendeleo ya michezo mkoani Geita kwa kusaidia uboreshaji wa miundombinu ya michezo, shule na huduma za afya katika jamii zinazozunguka mgodi
