Storm FM
Storm FM
9 September 2025, 5:58 pm

Kitendo hicho ni mfano wa kuigwa katika jamii kwani tukio hilo limeleta faraja kwa wagonjwa na hamasa kwa watoa huduma.
Na Mwandishi Wetu:
Kuelekea tamasha la Simba Day siku ya kesho, Mashabiki wa Simba tawi la Mkolani Manispaa ya Geita wamefanya matendo ya huruma katika Kituo cha Afya Nyankumbu kwa kufanya usafi na kutoa zawadi kwa wagonjwa mbalimbali waliyokuwepo kwenye kituo hicho.
Mwenyekiti wa tawi hilo Joseph Doto na msemaji wake Lukas Paul wakiwa kwenye zoezi hilo wamesema desturi hii imekuwa ikifanyika kila mwaka kuelekea tamasha la Simba Day ambapo mashabiki hutumia nafasi hiyo kugusa maisha ya wananchi kwa vitendo vya upendo na mshikamano.

Kwa upande wake Msemaji wa tawi la Yanga Mkolani aliyeambatana na mashabiki wa Simba SC kwenda kufanya matendo ya huruma kwenye kituo hicho amesema kitendo hicho ni mfano wa kuigwa katika jamii kwani tukio hilo limeleta faraja kwa wagonjwa na hamasa kwa watoa huduma.

Baadhi ya wagonjwa waliopatiwa Zawadi hizo Berdina Beda na Maria Brayson wamepongeza hatua hiyo huku Mganga mfawidhi wa Kituo hicho Dkt Irene Temba amesema wamefarijika sana kutembelewa na mashabiki wa Simba kituoni hapo kwani imeonyesha kuwa michezo ni zaidi ya burudani, ni chachu ya mshikamo na matumaini kwa jamii.