Storm FM

Yanga kurudi kama Mbogo kimataifa

3 August 2025, 3:40 pm

Msafara wa wanachama na mashabiki wa Yanga ukitembeza makombe Manispaa ya Geita. Picha na Mrisho Sadick

Klabu ya Yanga imeahidi kufanya vizuri kwenye michuano ya kimataifa msimu huu kuliko wakati wowote.

Na Mrisho Sadick:

Klabu ya Soka ya Yanga imeendelea kusherehekea mafanikio yake ya msimu wa 2024/25 kwa kutembeza makombe yake matano  katika mitaa mbalimbali ya Manispaa ya Geita mkoani Geita Jambo ambalo limevuta hisia za mashabiki wengi waliokuwa na hamasa kubwa kushuhudia mafanikio hayo ya kihistoria.

Msafara huo umeongozwa na msemaji wa klabu hiyo Ali Kamwe na Mkurugenzi wa wanachama, mashabiki na masoko, Ibrahim Samwel ambao wamekuwa kiungo muhimu kati ya klabu hiyo na mashabiki huku msemaji huyo akisema mwaka huu wamejipanga kufanya vizuri michuano ya Kimataifa kutokana na usajili mzuri ambao wameufanya.

Msemaji wa Yanga Ali Kamwe akizungumza na wanachama na mashabiki wa Yanga Mkoani Geita. Picha na Mrisho Sadick

Awali akitoa taarifa ya mwenendo wa wanachama katika matawi mratibu wa matawi ya Yanga mkoa wa Geita Rajabu Mohammed amebainisha changamoto mbalimbali zinazowakabili ikiwemo ukosefu wa ofisi ya mratibu wa matawi mkoa na usafiri huku mgeni rasmi katika sherehe hizo Hussein Makubi Mwananzara akiahidi kutatua changamoto hizo kwa awamu.

Wanachama na mashabiki wa Yanga wakiwa katika sherehe za ubingwa Manispaa ya Geita. Picha na Mrisho Sadick

Makombe yaliyotembezwa ni pamoja na Kombe la NBC, Ngao ya Jamii, Muungano Cup, CRDB  Cup pamoja na Toyota Cup.

Sauti ya Ripoti ya Stori hii na Mrisho Sadick