Storm FM

NMB kuendelea kuwainua wafanyabiashara Geita

31 July 2025, 8:28 pm

Katika picha kushoto ni Mkuu wa idara ya biashara wa NMB, katikati ni mwenyekiti wa NMB BUSINESS CLUB na mwisho ni kaimu meneja wa NMB Geita. Picha na Mrisho Sadick

Wafanyabiashara hao wameipongeza benki ya NMB kwa  kuwapatia mafunzo juu ya elimu ya fedha na mikopo

Na Mrisho Sadick:

Halmashauri ya Manispaa ya Geita Mkoani Geita imewataka wafanyabiashara kuhakikisha wanamiliki leseni halali za biashara huku ikisisitiza kuwa hatua hiyo itawasaidia kupata ulinzi wa kisheria na kuepuka usumbufu wa mara kwa mara kutoka kwa mamlaka husika.

Rai hiyo imetolewa na Afisa Biashara wa Manispaa ya Geita Mrisho katika semina ya wafanyabiashara iliyoandaliwa na Benki ya NMB kupitia mpango wake wa NMB Business Club katika ukumbi wa mikutano wa Otonde Plaza mjini Geita.

Watumishi wa NMB wakifuatilia mada mbalimbali zilizokuwa zikiwasilishwa kwenye NMB BUSINESS CLUB. Picha na Mrisho Sadick

Kwa upande wake Mkuu wa Idara ya biashara wa Benki ya NMB Alex Mgeni amewahamasisha wafanyabiashara hao kuendelea kushirikiana kwa karibu na benki hiyo ili kuiwezesha kuwa na uwezo wa kukopesha makampuni mengi kwa wakati mmoja na kusaidia kukuza uchumi wa ndani huku akisisitiza kuwa Benki hiyo kwasasa ndio Benki pekee nchini yenye mtaji mkubwa na uwezo wa kukopesha fedha nyingi kwa wakati mmoja.

Wafanyabiashara wa mkoa wa Geita wakifuatilia mada mbalimbali kwenye NMB BUSINESS CLUB mjini Geita. Picha na Mrisho Sadick

Wafanyabiashara hao akiwemo mwenyekiti wa NMB BUSINESS CLUB Mkoa wa Geita Michael Masusu na Recho Sospiter wameipongeza Benki ya NMB kwa  kuwapatia mafunzo juu ya elimu ya fedha na mikopo, ushuru na kodi, bima, masoko, pamoja na taratibu za kupata vibali vya biashara, huku wakihimizwa kuimarisha mahusiano ya kibiashara yatakayochochea maendeleo yao binafsi na jamii kwa ujumla.

NMB imesema lengo la mafunzo hayo, mbali na kutoa elimu, ni kuwashukuru wafanyabiashara kwa ushirikiano wao na pia kupata mrejesho wa changamoto wanazokumbana nazo ili kuboresha huduma zake na kuendelea kuwahudumia kwa ufanisi.

Sauti ya taarifa kamili ya stori hii na Ashura Ramadhani