

3 April 2025, 2:11 pm
Kutokana na ukosefu wa maeneo ya malisho Lwamgasa hali hiyo imegeuka mwiba mchungu kwa wafugaji wanaopitisha mifugo yao pori la hifadhi.
Na Mrisho Sadick:
Wafugaji wa Ng’ombe katika Kijiji Cha Lwamgasa wilayani Geita wamelalamikia vitendo vya kukamatwa nakutozwa pesa nyingi pindi mifugo yao inapoingia kwenye pori la hifadhi katika eneo hilo huku wakiiomba serikali kuliachia eneo hilo kwakuwa Kijiji hicho hakina sehemu nyingine ya malisho.
Wametoa kilio hicho April 02,2025 mbele ya Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Geita aliyeanza Ziara ya kusikiliza nakutatua kero za wananchi Mkoani humo ambapo wamesema Kijiji hicho kwa sehemu kubwa kimezungukwa na shughuli za uchimbaji wa madini ya dhahabu nakwamba hakuna eneo lingine kwa ajili ya kilimo na ufugaji tofauti na pori hilo.
Mkuu wa wilaya ya Geita Hashim Komba amesema pori hilo linaukubwa wa Hekta Elfu 28,000 nakwamba zimetengwa Hekta 10,000 kwa ajili ya kilimo na ufugaji wakati serikali ikiendelea kuweka utaratibu mzuri wa kuwagawia Wananchi rasmi.
Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Geita Nicholaus Kasendamila baada ya kusikiliza kero mbalimbali ikiwemo ya migogoro ya madini ,hali ya siasa katika kata hiyo , migogoro ya wakulima na wafugaji amemuagiza Mkuu wa wilaya Geita kuhakikisha anatatua kero zote zilizowasilishwa na wananchi kwenye mkutano huo kwa wakati.