

24 March 2025, 12:38 pm
“Tulikuwa tunapata changamoto sana ya kubeba wajawazito kutokana na ubovu wa barabara hii ambayo imetusumbua kwa muda mrefu” – Mwananchi
Na: Ester Mabula – Geita
Wananchi wa kitongoji cha Bukingwaminzi, Kijiji cha Narusunguti, kata ya Busonzo wilayani Bukombe mkoani Geita wamejitolea kutengeneza barabara kwa kutumia jembe la mkono katika kitongoji chao ili kuondoa changamoto ya muda mrefu ambayo ilikuwa ikiwakwamisha matumizi ya barabara hiyo
Wakizungumza leo March 24, 2025 wakiwa katika eneo la matengenezo ya barabara hiyo wameeleza kuwa hatua hiyo itawasaidia kuondokana na changamoto ya muda mrefu waliyokuwa wanaipitia hapo awali
Mwenyekiti wa kijiji cha Narusunguti Kasema Mashauri amewapongeza wananchi kwa hatua hiyo na kushauri vitongoji vingine ndani ya kijiji Narusunguti kata ya Busonzo kuiga mfano kwa kujitolea katika utatuzi wa changamoto.
Barabara hiyo inaunganisha Kijiji cha Nampalahala na Msonga na imekuwa ikitumiwa na wananchi wa kitongoji cha Bukingwamizi na vitongoji jirani kwaajili ya kusafirisha mazao na kupata huduma nyingine za kijamii.