

13 February 2025, 10:03 am
Katika hali ya kushangaza, binti ajinyonga na kufariki dunia baada kufeli katika mtihani wa Taifa wa kidato cha nne kwa kupata daraja 0.
Na: Edga Rwenduru – Geita
Binti Rabia Paul (19) muhitimu wa kidato cha nne katika shule ya sekondari Nyanza, mkazi wa mtaa wa Msalala road kata ya Kalangalala, manispaa ya Geita amefariki dunia baada ya kujinyonga kwa kile kinachodaiwa kuwa ni msongo wa mawazo kutokana na kufeli mtihani wa kidato cha nne kwa kupata daraja sifuri.
Akizungumza na Storm FM, Ali Bakari ambaye ni mjomba wa marehemu amesema chanzo kikubwa cha kufanya hivyo ni kufeli katika masomo yake.
Baadhi ya majirani wa familia hiyo wameeleza kusikitishwa na tukio hilo huku wakiikumbusha Jamii kuwa karibu zaidi na watoto wao.
Jeshi la polisi limethibitisha kutokea kwa tukio hilo ambapo Kamanda wa Jeshi la polisi mkoani Geita SACP Safia Jongo amesema tukio hilo limetokea Februari 11, 2025 majira ya saa 10 jioni ambapo mwili wake umekutwa ndani ya chumba alichokuwa akiishi.
Tayari mwili wa marehemu ulifanyiwa uchunguzi wa kitaalamu na kukabidhiwa kwa ndugu kwa ajili ya taratibu za maziko.