Storm FM

Wezi waiba na kuchinja ng’ombe wawili Nyankumbu

4 February 2025, 9:47 am

Ng’ombe aliyechinjwa na wezi katika shamba lililopo mtaa wa Nyankumbu. Picha na Edga Rwenduru

Matukio ya mifugo aina ya ng’ombe kuibiwa na kuchinjwa nyakati za usiku yameendelea kuacha maswali kwa wananchi katika mitaa mbalimbali ya manispaa ya Geita.

Na: Edga Rwenduru – Geita

Wakazi wa mtaa wa Elimu kata ya Nyankumbu halmashauri ya manispaa ya Geita wamelalamikia kukithiri kwa matukio ya wizi wa mifugo aina ya ng’ombe ambapo mifugo hiyo inakutwa imechinjwa na wezi na kuondoka na nyama huku wakiiomba serikali kuchukua hatua za haraka ili kunusuru mifugo yao.

Wakazi wa mtaa wa Elimu wakiwa katika eneo ilipokuwa ng’ombe imechinjwa. Picha na Edga Rwenduru

Wakizungumza na Storm FM wakazi wa eneo hilo wamesema matukio hayo yamezidi kuongezeka huku wakiliomba jeshi la polisi kuwasaidia kwani licha ya jitihada zinazofanywa na polisi jamii wa mtaa huo bado watuhumiwa wamekuwa wakirejea mtaani na kuendelea kufanya uhalifu.

Sauti ya wananchi
Mwenyekiti wa mtaa wa Elimu Hassan Mshole akizungumza na Storm FM. Picha na Edga Rwenduru

Mwenyekiti wa mtaa wa Elimu Hassan Mshole amesema tayari wameanza mikakati ya kuhakikisha wanapambana na matukio hayo ya wizi kwa kuitisha mikutano ya hadhara na kupiga kura ili kutambua ni watu gani wanaotekeleza matukio hayo huku akiwaomba wananchi kutoa ushirikiano kwa jeshi la polisi pindi wanapoitajika kwaajili ya kutoa ushahidi.

Sauti ya mwenyekiti mtaa wa Elimu Hassan Mshole

Diwani wa kata ya Nyankumbu John Mapesa ameliomba Jeshi la polisi kufuatilia matukio hayo kwani inaonekana vijana wanaotekeleza matukio hayo ya kuchinja mifugo ya watu na kuondoka na nyama wanapata oda kutoka kwenye migahawa na huuza nyama hiyo kwa bei nafuu ikilinganishwa na zile za buchani.

Sauti ya Diwani kata ya Nyankumbu John Mapesa

Storm FM inafanya jitihada za kumtafuta Kamanda wa Jeshi la polisi mkoa wa Geita ili kuweza kufahamu mikakati zaidi katika kukomesha matukio haya.