Storm FM
Storm FM
20 November 2025, 5:16 pm

Mamlaka za usalama majini zimeahidi kuendelea na ukaguzi wa mara kwa mara, kutoa mafunzo na kusisitiza matumizi ya vifaa vya usalama majini.
Na Mrisho Sadick:
Vifo vitokanavyo na ajali za majini wilayani Chato Mkoani Geita vimepungua kwa asilimia kubwa baada ya wavuvi kuanza kutumia vifaa vya usalama kwenye mitumbwi na boti zao.
Wavuvi katika mwalo wa Chato Beach wilayani Chato Mkoani Geita wamesema elimu ya matumizi ya vifaa vya usalama majini imechangia kwa kiasi kikubwa kupunguza ajali za majini zilizokuwa zikisababisha vifo kwa wavuvi.

Shirika la uwakala wa meli Tanzania TASAC kupitia kwa Godfrey Chegere Afisa Mfawidhi Mkoa wa Geita amesema wameendelea kutoa Elimu ya usalama majini kwa kushirikiana na Halmashauri ya wilaya ya Chato imeokoa wavuvi wengi kutopoteza maisha.

Mkuu wa wilaya ya Chato Mkoani Geita Louis Bura ametoa angalizo kwa wavuvi kuendelea kusajili boti zao na kuchukua tahadhali wakati wakitekeleza majukumu yao ziwani.