Storm FM

Mgombea ubunge CCM Geita mjini awafikia wajasiriamali Nyankumbu

27 September 2025, 12:42 am

Mgombea ubunge jimbo la Geita mjini kwa tiketi ya CCM mhandisi Chacha Wambura akizungumza na wananchi na wajasiriamali (hawapo pichani) katika soko la Nyankumbu. Picha na mwandishi wetu
Mhandisi Chacha Wambura, mgombea ubunge jimbo la Geita mjini akisalimiana na mwananchi katika soko la Nyankumbu. Picha na mwandishi wetu
Wananchi na wajasiriamali soko la Nyankumbu wakimsikiliza mgombea ubunge jimbo la Geita mjini (CCM) mhandisi Chacha Wambura. Picha na mwandishi wetu
Mgombea ubunge (CCM) mhandisi Chacha Wambura akinunua bidhaa kutoka kwa mjasiriamali soko la Nyankumbu. Picha na mwandishi wetu
Wajasiriamali soko la Nyankumbu wakimsikiliza mgombea udiwani wa kata hiyo Paschal Sukambi. Picha na mwandishi wetu
Mgombea ubunge jimbo la Geita mjini kwa tiketi ya CCM akiteta jambo na mwanachama wa CCM. Picha na mwandishi wetu
Eng. Chacha Wambura, mgombea ubunge (CCM) jimbo la Geita mjini akiangalia bidhaa za wajasiriamali. Picha na mwandishi wetu

“Ilani ya CCM kwa mwaka 2025 imeainisha maeneo muhimu yanayogusa maisha ya wananchi kwenye afya, elimu, miundombinu pamoja na biashara” – Mhandisi Chacha

Na:Ester Mabula

Mgombea ubunge wa Jimbo la Geita mjini kupitia tiketi ya CCM Mhandisi Chacha Wambura katika mwendelezo wa kampeni zake leo Septemba 26, 2025 ametembelea soko la Nyankumbu ambapo amesikiliza kero na changamoto mbalimbali zinazowakabili katika shughuli zao za kila siku.

Miongoni mwa changamoto zilizotajwa na wajasiriamali wa soko hilo ni pamoja na ukosefu wa maji ya kutosha kwenye vyoo vya soko, kutokuwepo kwa eneo maalum la kushushia mizigo, tatizo la mitaro ya maji, pamoja na malalamiko juu ya tozo za vizimba.

Chacha amewahakikishia wajasiriamali hao kuwa CCM imeweka kipaumbele kikubwa katika kuhakikisha masoko yote nchini yanakuwa na mazingira rafiki kwa wafanyabiashara ili waweze kufanya shughuli zao kwa usalama na tija.

Ameahidi kwamba, akipewa ridhaa ya kuwa Mbunge wa Jimbo la Geita Mjini, atashirikiana kwa karibu na viongozi wa serikali na taasisi husika kuhakikisha changamoto hizo zinatafutiwa majibu ya kudumu na soko la Nyankumbu linajengwa kwa viwango bora kulingana na mipango ya serikali.

Aidha, Eng. Chacha Mwita Wambura amewaomba wafanyabiashara wa Nyankumbu na wananchi wa Geita kwa ujumla kumpa kura katika uchaguzi mkuu ujao ili aweze kushirikiana nao kwa vitendo katika kuimarisha biashara zao na kuendeleza maendeleo ya Geita.