Storm FM

Wanawake sasa wanachimba madini kitaalam Geita

20 September 2025, 8:37 pm

Katibu Mkuu TAWOMA Salma Ernest akizungumza kwenye semina. Picha na Mrisho Sadick

Serikali imenunua mitambo 15 kwa ajili ya wachimbaji wadogo na itaendelea kuwaunga mkono kila hatua

Na Mrisho Sadick:

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan ametoa leseni 17 na vifaa vya kisasa vya uchimbaji wa madini ya dhahabu kwa vikundi vya wanawake wanaofanya shughuli za uchimbaji wa madini ya dhahabu mkoani Geita.

Katibu Mkuu wa Chama cha Wachimbaji Madini Wanawake Tanzania (TAWOMA) Salma Ernest amebainisha hayo kwenye Semina maalumu kwa wachimbaji Wanawake katika maonesho ya nane ya Teknolojia na Uwekezaji katika sekta ya madini kwenye viwanja vya Dkt Samia Suluhu Hassan Manispaa ya Geita nakwamba hatua hiyo itawasaidia wanawake kufanya shughuli zao kitaalamu tofauti na ilivyokuwa awali ambapo baadhi walitegemea imani za kishirikina katika uchimbaji.

Washiriki kutoka makundi mbalimbali wakiwa kwenye semina. Picha na Mrisho Sadick
Sauti ya Katibu Mkuu TAWOMA

Baadhi ya wachimbaji wadogo Wanawake wa Mkoa wa Geita akiwemo paskazia Philbati na Asia Masimba wamesema kutolewa kwa vifaa hivyo na mafunzo mbalimbali ambayo wanaendelea kuyapata kumewafanya kuongeza ujuzi na ufanisi katika shughuli hizo.

Sauti ya Wachimbaji Wanawake

Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Madini la Taifa (STAMICO), Venas Mwase, amesema serikali imenunua mitambo 15 kwa ajili ya wachimbaji wadogo na itaendelea kuwaunga mkono.

Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Madini la Taifa (STAMICO), Venas Mwase akizungumza kwenye semina. Picha na Mrisho Sadick
Sauti ya Mkurugenzi STAMICO

Maonesho ya 8 ya Teknolojia na Uwekezaji katika Sekta ya Madini yanafanyika kuanzia Septemba 18–28, 2025 katika Viwanja vya Dkt. Samia Suluhu Hassan, Bombambili, Manispaa ya Geita, yakitoa fursa ya kunufaika na teknolojia za kisasa kwa wachimbaji wote.