Storm FM
Storm FM
15 September 2025, 10:00 am

Upatikanaji wa magari hayo ni juhudi za Serikali ya Awamu ya Sita katika kuboresha mazingira ya kazi ya vyombo vya ulinzi na usalama nchini.
Na Mrisho Sadick:
Jeshi la Polisi Mkoa wa Geita limepokea magari 15 mapya kwa lengo la kuongeza ufanisi, kuboresha utendaji kazi na kuimarisha uwajibikaji katika kulinda usalama wa wananchi na mali zao.
Makabidhiano ya magari hayo yamefanyika kwenye viwanja vya Polisi Manispaa ya Geita, ambapo Mkuu wa Mkoa wa Geita, Martine Shigela, amewakabidhi rasmi viongozi wa Jeshi la Polisi mkoani humo wakiongozwa na Kamanda wa Polisi Mkoa SACP Safia Jongo.

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Geita amesema kupatikana kwa magari hayo ni juhudi za Serikali ya Awamu ya Sita katika kuboresha mazingira ya kazi ya vyombo vya ulinzi na usalama nchini, hatua ambayo imeendelea kuongeza ari na ufanisi wa askari katika kutekeleza majukumu yao.

Sambamba na utoaji wa vitendea kazi hivyo, Serikali pia imeendelea kuchukua hatua za kuboresha maslahi ya askari, ikiwemo kuwapandisha vyeo na kuimarisha huduma zao za kijamii tofauti na wakati mwingine huku Mkuu wa Mkoa wa Geita Martine Shigela akilipongeza Jeshi la Polisi Mkoani humo kwa kudhibiti matukio mbalimbali ya kihalifu, hususan vitendo vya wizi wa mifugo vilivyokuwa vimekithiri.