Storm FM
Storm FM
12 May 2025, 2:42 pm

Mwenyekiti wa Chama cha wachimba madini mkoa wa Geita (GEREMA) Ndg. Titus Kabuo amesema dhumuni kubwa la kongamano hilo ni kumpongeza Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuiboresha sekta ya madini na kuweka mazingira rafiki ya uchimbaji na ufanyaji biashara.
Na: Ester Mabula:
Wachimbaji na wafanyabiashara wa Madini wa Mkoa wa Geita wamempongeza Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa mafanikio makubwa yaliyopatikana kupitia sekta ya madini katika kipindi cha miaka minne ya uongozi wake.
Pongezi hizo zimetolewa jana Mei 11, 2025 kwenye mkutano wa hadhara ulioandaliwa na wachimbaji hao katika eneo la mnada wa zamani Katoro mkoani Geita kwa lengo la kumpongeza Rais Samia kwa mafanikio yaliyopatikana kupitia sekta ya madini.
Mgeni rasmi Waziri wa Madini Mh. Anthony Mavunde ameyataja mafanikio ya Rais Samia kuipaisha sekta ya madini ikiwemo kuongezeka kwa makusanyo ya maduhuli kuelekea lengo la kukusanya shilingi Trilioni moja na upatikanaji wa mitambo ya kuchoronga 15 kwaajili yaa wachimbaji wadogo.

Mkuu wa mkoa wa Geita Mhe. Martin Shigela amesema Mkoa wa Geita umejipanga kuchochea shughuli za madini kwa kuboresha mazingira ya uchimbaji ili kukuza uchumi wa wananchi wa mkoa wa Geita kupitia upatikanaji wa Leseni zaidi ya 5308 na mitambo.
Vikundi vya wanawake wachimbaji na wanaojihusisha na biashara ya madini wametoa pongezi kwa Rais Samia kwa kuendelea kutoa kipaumbele pia kwa wanawake na hivyo kuchochea maendeleo katika sekta ya madini kwa ujumla.
