

1 March 2025, 11:24 am
Mamlaka ya mapato Tanzania mkoa wa Geita imeendelea kurejesha shukrani kwa Jamii kwa kuwakumbuka watu wenye mahitaji mbalimbali kupitia misaada.
Na: Edga Rwenduru – Geita
Mamlaka ya mapato Tanzania (TRA) mkoa wa Geita imetoa msaada wa vifaa tiba katika hospitali ya manispaa ya Geita na mahitaji kwa watoto wenye mahitaji maalumu katika kituo cha Moyo wa huruma kilichopo Mbugani mjini Geita lengo likiwa ni kurudisha shukrani kwa Jamii.
Shughuli ya utoaji wa misaada hiyo imefanyika Februari 27, 2025 ambapo Meneja wa TRA mkoa wa Geita Helirehema Kimambo amekabidhi vifaa tiba vyenye thamani ya zaidi ya milioni 4 katika hospitali ya manispaa ya Geita na mahitaji kwa watoto wenye mahitaji maalumu yenye thamani ya zaidi ya milioni moja na laki tano.
Kaimu mganga mfawidhi wa hospitali ya Manispaa ya Geita Dkt. Sospeter Marwa amesema vifaa hivyo vitakuwa msaada mkubwa kwao kama watumishi na wagonjwa wanaopata huduma katika hospitali hiyo.
Kwa upande wake Madam Edwick Ndunguru, mwalimu mkuu wa shule ya msingi Mbugani amesema shule hiyo ina wanafunzi 1876 ambapo wanafunzi wenye mahitaji maalumu ni 164 ambapo ameishukuru TRA Kwa kuwapatia msaada huo huku akizidi kuwaomba wadau kuzidi kujitokeza kuwasaidia.