Storm FM

GGML yakabidhi pikipiki 50 kwa Jeshi la polisi Geita

22 October 2024, 5:38 pm

Waziri wa mambo ya ndani ya nchi mhandisi Hamad Yusuph Masauni (kati) akikata utepe kuashiria makabidhiano ya pikipiki kwa Jeshi la polisi. Picha na Ester Mabula

GGML imeendelea kushirikiana na serikali katika kufadhili shughuli mbalimbali za maendeleo mkoani Geita ikiwa ni ajenda yao ya kunufaisha Jamii inayozunguka mgodi huo.

Na: Ester Mabula – Geita

Kampuni ya Geita Gold Mining Limited (GGML) imekabidhi pikipiki 50 kwa Jeshi la polisi mkoa wa Geita zenye thamani ya shilingi milioni 175 ikiwa ni sehemu ya kuunga mkono juhudi za kuimarisha usalama na ulinzi wa mkoa.

Hafla ya makabidhiano imefanyika katika ukumbi wa bwalo la polisi uliopo halmashauri ya mji wa Geita ikihudhuriwa na viongozi mbalimbali wa kitaifa, viongozi wa mkoa, viongozi wa GGML pamoja na watendaji wa Jeshi la polisi.

Baadhi ya polisi kata wakiwa juu ya pikipiki walizokabidhiwa na GGML. Picha na Ester Mabula

Mgeni rasmi ambaye ni Waziri wa mambo ya ndani ya nchi Mhandisi Hamad Masauni ameupongeza mgodi wa GGML kwa kuendelea kushirikiana na serikali katika kurahisisha utekelezaji wa majukumu akieleza kuwa serikali ya awamu ya sita inaendelea kuweka mazingira rafiki ya ufanyaji kazi kwa Jeshi la polisi.

Sauti ya waziri Masauni
Waziri wa mambo ya ndani ya nchi mhandisi Hamad Masauni akizungumza katika hafla ya makabidhiano ya pikipiki kwa Jeshi la polisi. Picha na Ester Mabula

Makamu wa Rais mwandamizi wa Anglo Gold Ashanti Afrika Terry Strong amesema GGML inaendelea kutambua kazi kubwa inayofanywa na polisi na hivyo wataendeleza ushirikiano ili kurahisisha utendaji kazi huku Afisa mwandamizi wa mahusiano Gilbert Moria akieleza kuwa GGML itaendelea kunufaisha Jamii inayozunguka mgodi huo.

Sauti ya viongozi GGML
Makamu wa Rais mwandamizi wa Anglo Gold Ashanti Afrika Terry Strong akizungumza katika hafla ya makabidhiano ya pikipiki kwa Jeshi la polisi. Picha na Ester Mabula

Mkuu wa mkoa wa Geita Martine Shigela ameipongeza GGML kwa kuendelea kutoa ufadhili katika miradi mbalimbali ya maendeleo na kuahidi kuendeleza kudumisha ushirikiano kwa maendeleo ya mkoa wa Geita na Taifa kwa ujumla.

Sauti ya RC Geita
Baadhi ya viongozi wa mkoa wa Geita wakitoa heshima kwa waziri wa mambo ya ndani mhandisi Hamad Masauni baada ya kuwasili mkoani Geita. Picha na Ester Mabula

Baadhi ya askari polisi wamesema pikipiki hizo zitawasaidia katika utekelezaji wa majukumu yao ya kila siku sambamba na kudumisha usalama wa raia.

Sauti ya Askari polisi

GGML imeendelea kudumisha ushirikiano na serikali ambapo kupitia miradi ya uwajibikaji wa kampuni kwa Jamii (CSR) imekuwa ikitenga shilingi Bilioni 1.9 kila mwaka kwaajili ya utekelezaji wa miradi.