Nuru FM

Wananchi Ulanda waomba kukarabatiwa barabara

23 July 2026, 10:30

Mbunge wa Jimbo la Kalenga mwenye Kofia akizungumza na wananchi wa Kijiji cha Lupalama Kata ya Ulanda. Picha na Hafidh Ally

Wananchi wa Kata ya Ulanda wamesema kuwa barabara inayounganisha Kata ya Ulanda na maeneo jirani haijaimarishwa kwa kujengwa makaravati.

Na Hafidh Ally

Wananchi wa Kata ya Ulanda, Jimbo la Kalenga, Wilaya ya Iringa, wameiomba Serikali kuboresha miundombinu ya barabara za vijiji vya kata hiyo, wakisema hali ya barabara imeendelea kuwa kero kubwa, hususan kipindi cha mvua.

Wakizungumza wakati wa ziara ya kikazi ya Mbunge wa Jimbo la Kalenga, Mheshimiwa Jackson Kiswaga, wananchi wa vijiji vya Mwambao, Weru, Lupalama na Kibebe walisema kuwa, licha ya utekelezaji mzuri wa miradi mbalimbali ya maendeleo, barabara inayounganisha Kata ya Ulanda na maeneo jirani bado haijaboreshwa kwa kujengwa makaravati, jambo linalosababisha magari kushindwa kupita wakati wa mvua.

Sauti ya Wananchi Ulanda

Aidha, wananchi hao walimuomba Mbunge wao kueleza ni lini barabara hizo zitafanyiwa matengenezo, wakisema walipatiwa ahadi hiyo tangu mwaka 2019 lakini hadi sasa haijatekelezwa. Walisema hali hiyo pia imekuwa ikiwasababishia wanafunzi kupata shida kufika shuleni, hasa kipindi cha mvua.

Sauti ya Wananchi Ulanda

Akijibu changamoto hiyo, Mbunge wa Jimbo la Kalenga, Mheshimiwa Jackson Kiswaga, alisema jimbo hilo hupokea takribani shilingi bilioni 3.5 kila mwaka kwa ajili ya matengenezo ya zaidi ya kilometa 900 za barabara.

Hata hivyo, alisema fedha hizo hazitoshelezi kutekeleza mahitaji yote yaliyopo, hivyo Serikali hulazimika kuweka kipaumbele kwenye barabara zilizoharibika zaidi na zisizopitika kabisa.

Sauti ya Mbunge Kiswaga

Kiswaga alifafanua kuwa Serikali imeiomba mamlaka husika kufanya tathmini upya ya mtandao wa barabara ili kuongeza fedha za matengenezo na kuboresha huduma hiyo.

Alisema mkakati wa muda mrefu ni kubadilisha barabara nyingi za udongo kuwa za changarawe ili kupunguza gharama za matengenezo na kuongeza uimara wake kwa muda mrefu.