Nuru FM
Nuru FM
11 November 2025, 11:38

Mradi wa Iringa Commercial Complex unatarajiwa kukuza uchumi wa Iringa.
Na Hafidh Ally
Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Mhe. Herry James, amepongeza maendeleo makubwa ya ujenzi wa mradi wa Iringa Commercial Complex, unaotekelezwa mjini Iringa kwa gharama ya shilingi bilioni 9.7.
Mhe. Herry James amesema ameridhishwa na kasi ya utekelezaji wa ujenzi huo wa ghorofa nne, unaotarajiwa kukamilika ndani ya mwaka mmoja na miezi sita.
Aidha, Mkuu wa Mkoa amewahimiza wananchi wa Iringa kuchangamkia fursa zitakazotokana na mradi huo, ambao utajumuisha maduka ya biashara, maduka makubwa (supermarkets), kumbi za burudani (night clubs) na nyumba za makazi.

Kwa upande wake, Meneja wa Shirika la Nyumba Mkoa wa Iringa, Bi. Ester Magese, amesema mradi huo pia utatoa fursa kwa wananchi kununua nyumba 52 zitakazojengwa kwa ajili ya makazi.
Nao wananchi Mkoani Iringa ambao wamepata ajira kupitia mradi huo, wameeleza kuwa ujenzi umefikia hatua ya asilimia 20 hadi sasa, huku wakiishukuru serikali kwa kuleta mradi huo ambao utawahusisha wananchi wote kupata huduma mara baada ya kukamilika.
Mradi wa Iringa Commercial Complex unatarajiwa kuwa miongoni mwa miradi ya kisasa itakayobadilisha sura ya Mji wa Iringa na kuchochea ukuaji wa uchumi wa mkoa huo.
