Nuru FM
Nuru FM
14 April 2026, 19:57

Shirika la IDYDC limefanikiwa kuwapatia maji ya Mkopo wananchi wa Mgera ambao walikuwa wakitumia umbali mrefu kufuata huduma ya maji Mabondeni.
Na Hafidh Ally
Jumla ya Kaya 18 za Kijiji cha Mgera Kilichopo Kata ya Kiwele Wilaya ya Iringa zimenufaika na Mradi wa maji ya Mkopo kutoka shirika la IDYDC.
Wakizungumza na Nuru FM baadhi ya wananchi kutoka Kaya zilizonufaika na Mradi wa kuunganishiwa Maji kupitia Mamlaka ya Maji safi na Usafi wa Mazingira Iruwasa chini ya Shirika hilo, wamesema kuwa walikuwa wanatumia gharama kubwa kununua maji ambapo kwa siku kila kaya walikuwa wakitumia kuanzia shilingi elfu 1 mpaka elfu 6.

Aidha wananchi hao wamesema kuwa kabla ya kupata huduma ya maji safi ya Bomba walikuwa wakitumia maji ambayo si safi na salama kwao.
Kwa upande wake Afisa Mtendaji wa Kijiji cha Mgera Jimmy Changaka amelishukuru shirika la IDYDC kwa kuwalipia fedha za Mkopo wa huduma ya maji ambayo ilikuwa changamoto kwa wananchi hao.

Denis Mdule Ni Mwenyekiti wa Kitongoji cha Mapinduzi Kilichopo Kijiji Cha Mgera amesema kuwa kabla ya kufungiwa huduma hiyo ya maji wananchi wake walikuwa wakiyafuata maji mbali katika mito na visima.
Meneja wa Mradi wa kusaidia kaya maskini kupata huduma ya kuunganishiwa maji kutoka shirika la IDYDC Ndugu Castory David Amesema kuwa Mradi huo unaofadhiliwa na serikali ya Ujerumani (BMZ) kupitia shirika la Foundation North-South Bridge na AKEH umelenga kuhakikisha kaya zisizokuwa na maji zinapata bila riba.