Nuru FM

Wafanyabiashara Kihesa waomba wakarabatiwe soko

7 March 2024, 3:29 pm

Muonekano wa Soko la Kihesa lililopo Manispaa ya Iringa. Picha na Godfrey Mengele

Licha ya Viongozi Kutoa ahadi kuhusu ukarabati wa Soko hilo lakini utekelezaji wake umekuwa Mgumu.

Na Godfrey Mengele

Wafanyabiashara wa soko la Kihesa maarufu kama kihesa sokoni lililopo halmashauri ya Manispaa ya Iringa wameitaka serikali kuwajengea soko lenye hadhi ya kufanyia biashara ili kukabiliana na ubovu wa miundombinu iliyopo sasa.

Wakizungumza na Nuru Fm kupitia kipindi cha Nyambizi wafanyabiashara hao wamesema kuwa ni muda mrefu sasa wamekuwa wakipewa ahadi kutoka kwa viongozi mbalimbali juu ya kuwajengea soko lakini zimekuwa ni ahadi zisizo tekelezeka.

“Tunawaomba hao Viongozi wake kutekeleza ahadi ya Kutupatia soko lenye moundombinu rafiki, kwa kweli tunateseka hasa kipindi Cha Mvua” Walisema wafanyabiashara hao

Soko la kihesa linajumla ya wafanyabiashara zaidi ya 100 lakini changamoto kubwa wanayokabiliana nayo ni ubovu wa miundombinu ya soko ambapo kwani vibanda vilivyopo katika soko hilo ni vya kuezekwa na mabanzi na si vizimba kama ilivyo katika masoko mengine.

Bidhaa zinazouzwa katika soko hilo ni malimbichi wafanyabiashara hao ambao wengi wao wanazaidi ya miaka 20 wakifanya biashara eneo hilo wanasema msimu wa mvua katika kulinda bidhaa zao inawalazimu kutumia mifuko migumu ya lailon isiyopitisha maji ili kunusuru kutoharibika kwa mali hizo.

Diwani wa kata ya kihesa Ndg July Sawani amekiri wazi kuwa ni kitambo kirefu wafanyabiashara hao wamekuwa wakipitia changamoto ya uchakavu wa miundombinu hivyo kupitia Mbunge wa Jimbo la Iringa Mjini Mhe Jesca Msambatavangu tayari fedha imepatikana kutoka Word Bank na tathimini imefanyika ili kujenga soko hilo ambalo litakuwa na vizimba 300 ambapo ujenzi utaanza mwezi wa 6 mwaka huu.