Mafinga Mji wapongeza ujenzi wa barabara
29 May 2026, 09:07

Na Hafidh Ally
Wananchi Halmashauri ya Mji Mafinga wameipongeza serikali kwa kufanya ujenzi wa barabara yenye urefu wa kilomita 1.3 unaotekelezwa na Serikali kwa gharama ya shilingi milioni 700 ambao umeleta manufaa makubwa kwa jamii.
Wakizungumza mara baada ya Barabara hiyo kukaguliwa na kuwekwa jiwe la msingi na Kiongozi wa Mbio za Mwenge wa Uhuru, wananchi hao wamesema kuwa itarahisisha usafiri na usafirishaji, kuongeza fursa za biashara pamoja na kuboresha muonekano wa mji huo.

Kwa upande wake Mbunge wa Jimbo la Mafinga Mjini Dickson Lutevele Villa amesema kuwa ujenzi wa barabara katika jimbo lake utasaidia kuondoa kero kwa wananchi wanayokutana nayo hasa wakati wa mvua.
Naye KIONGOZI wa Mbio za Mwenge wa Uhuru Kitaifa 2026, Wazo Mwang’onda amesema kuwa serikali imedhamiria kuhakikisha maeneo yote yanakuwa na barabara zinazopitika wakati wote.