Nuru FM

CAG abaini kitu mita za Tanesco

28 March 2024, 9:45 pm

Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG), Charles Kichere akikabidhi ripoti kwa Rais Samia Suluhu Hassan. Picha na Habari leo.

Ripoti ya CAG imebaini kuwa mita zaidi ya 100,000 kati ya mita 602,266 zilibadilishwa kabla ya kipindi cha uhai wa matumizi yake kuisha.

Na Mwandishi wetu

RIPOTI ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG), Charles Kichere, kwa mwaka wa fedha wa 2022/23, imeibua madudu kwa Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO)

Akisoma ripoti hiyo leo Machi 28, 2024 Ikulu Chamwino mjini Dodoma, CAG Charles  Kichere amesema ukaguzi wake umebaini dosari katika suala la ubadilishaji wa mita.

Amesema mita zaidi ya 100,000 kati ya mita 602,266 zilibadilishwa kabla ya kipindi cha uhai wa matumizi yake kuisha, wakati mita 13,493 zilibadilishwa ndani ya mwaka mmoja baada ya kufungwa, huku zaidi ya mita 90,000 zikiwa na muda mfupi wa matumizi kinyume na muda unaokubalika wa miaka 20.

“Kubadilisha mita mapema kunasababisha gharama kubwa kwa shirika letu, napendekeza wizara ichunguze sababu za TANESCO kubadilisha mita mapema na kuchukua hatua ili kupunguza gharama za uzalishaji,” amesema Kichere.