Nuru FM

Wanahabari wapewa mafunzo ya radio portal

7 March 2024, 10:09 am

Baadhi ya wanahabari wakiwa katika mafunzo jijini Dar es Salaam. Picha na Markku Liukkonen.

Mafunzo ya kuwajengea uwezo wanahabari ili waweze kuandaa maudhui bora mtandaoni hasa kupitia radio portal.

Na Hafidh Ally

Waandishi wa habari kutoka radio jamii zilizopo chini ya mtandao wa TADIO wamepewa mafunzo ya namna ya kuchapisha na kutuma maudhui kupitia radio portal.

Mafunzo hayo ya siku mbili yameanza leo March 7 hadi march 8 yamefanyika katika ukumbi wa Jamirex Hotel iliyopo Mwenge jijini Dar es Salaam.

Mkufunzi wa mafunzo hayo kutoka shirika la Vikes Peik Johansson alianza kwa kutaka wanahabari wanaosimamia radio portal kuelezea jinsi ilivyoweza kuleta mabadiliko na changamoto zilizopo huku akisisitiza kuwa mtandao huo husaidia kuongeza wasikilizaji.

Nao baadhi ya wanahabari wanaopata mafunzo hayo wamesema kuwa radio portal imesaidia kusambaza maudhui ya kijamii na kuwafikia walaji wengi.

“Kwa sasa watumiaji wengi wa Mitandao ya kijamii wameongezeka kwa sababu tumekuwa tukipost story zetu kwenye portal” alisema mmoja wa waandishi.

Hata hivyo changamoto kubwa iliyowasilishwa katika uendeshaji wa radio portal katika uchapishaji wa maudhui ni pamoja na ukosefu wa mtandao, changamoto ya umeme, ukosefu wa bajeti kwa ajili ya kununua bando.

Aidha wamewaomba wasimamizi wa vituo vya radio jamii kuwekeza nguvu katika upatikanaji wa majenereta (nishati mbadala) ili kusaidia radio portal kuwa hewani muda wote.