Mazingira FM
Mazingira FM
8 January 2026, 10:56 am

Upotevu wa maji kwenye mamlaka ya maji Bunda kwa sasa ni asilimia 31 kati 45 iliyokuwepo awali hali inayopelekea kupoteza zaidi ya shilingi milioni 600 kwa mwaka.
Na Adelinus Banenwa
Serikali imesema haitaanzisha miradi mingine mipya ya maji hadi pale inayoendelea kutekelezwa itakapokamilika.
Hayo yamesemwa na naibu waziri wa maji Mhe Kundo Andrew Mathew wakati wa uwekaji wa jiwe la msingi katika ujenzi wa mradi wa kuzuia upotevu wa maji kutoka Migungani hadi mlima Kaswaka
Mhe Kundo amesema ni dhamira ya serikali kuhakikisha kila mwananchi anapata huduma ya maji safi na salama kwa utoshelevu ndiyo maana inatekeleza miradi mikubwa ukiwemo mradi huo wenye thamani ya zaidi ya Bilion 1.49

Aidha Mhe kundo amesisitiza watumishi wa wizara ya maji kuacha tabia ya kuwambia wananchi miradi ipo kwenye mchakato badala yake wawaambie ukweli kama mradi upo asilimia kadhaa ili kuondoa maswali na malalamiko kwa wananchi.
Akizungumza katika taarifa kutoka mamlaka ya maji safi na usafi wa mazingira Bunda BUWSSA mkurugenzi wa BUWSSA Bi Esther Gilyoma amesema mradi huo unatekelezwa kwa urefu wa kilometa 4.2 kwa thamani ya shilingi bilion 1.49 na kati ya hizo tayari kilometa 2.1 tayari mtaro umechimbwa na mradi umefikia asilimia 50 na mkandarasi anaendelea na mradi.
Bi Esther amesema changamoto ya upotevu wa maji kwenye mamlaka hiyo kwa sasa ni asilimia 31 kati 45 iliyokuwepo awali hali inayopelekea kupoteza zaidi ya shilingi milioni 600 kwa mwaka.

Aidha Bi Esther amesema kama BUWSSA wanafanya jitihada za kubadilisha miundombinu chakavu, kuondosha mita za maji sumbufu, na kutoa elimu kwa wananchi ili kulinda miundombinu iliyopo ikiwepo kuepuka wizi wa maji lengo ni kupunguza upotevu wa maji hadi viwango vya kimataifa ambavyo ni asilimia 20.
Awali akiwasilisha kero za Wananchi Mbunge wa Bunda mjini Esther Bulaya amesema mradi huo umegusa kilio chake cha muda mrefu cha kuuondoa mji wa Bunda katika orodha ya maeneo ambayo yana upotevu mkubwa wa maji.

Amesema hana mashaka na usimamizi wa Mkurugenzi wa Mamlaka ya Maji Bunda, Bi. Esther Gilyoma kwani ameonesha uwezo mkubwa wa kupambana tangu awali kupunguza upotevu kutoka Silimia 45 hadi 31 za sasa.