Mazingira FM
Mazingira FM
18 October 2025, 7:41 pm

Wanafunzi 195 wamesajiliwa kufanya Mtihani wa Taifa, ambapo wasichana ni 101 na wavulana 94.
Na Adelinus Banenwa
Jumla ya wanafunzi 195 wanatarajiwa kuhitimu masomo yao ya Kidato cha Nne mwaka 2025 katika Shule ya Sekondari Bunda Day, ambayo imefanya Mahafali yake ya 32 hivi karibuni. Hafla hiyo imehudhuriwa na wazazi, walimu, wanafunzi pamoja na wageni mbalimbali waalikwa.
Akizungumza wakati wa hafla hiyo, Mkuu wa shule, Bw. Charles Somba, amesema kuwa wanafunzi 195 wamesajiliwa kufanya Mtihani wa Taifa, ambapo wasichana ni 101 na wavulana 94. Aidha, ameeleza kuwa kwa miaka miwili mfululizo, shule hiyo imepata ufaulu wa asilimia 100, bila mwanafunzi yeyote kupata daraja sifuri.
Hata hivyo, pamoja na mafanikio hayo, Bw. Somba ametaja changamoto kadhaa zinazokabili shule hiyo, zikiwemo ukosefu wa uzio katika bweni la wasichana na upungufu wa walimu wa masomo ya sayansi na sanaa, hali ambayo inahitaji msaada kutoka kwa wadau wa elimu.

Kwa upande wao, wahitimu kupitia risala yao, wamelalamikia ukosefu wa kompyuta, pamoja na kutokamilika kwa maktaba na maabara ya kompyuta, wakisema hali hiyo inarudisha nyuma maendeleo yao ya kitaaluma.
Akizungumza kwa niaba ya mgeni rasmi, Mhandisi Kambarage Wasira, Bw. Jakson Lazaro ameipongeza shule hiyo kwa matokeo mazuri, na kuahidi kuwa wao kama wadau wa maendeleo wataendelea kushirikiana na uongozi wa shule katika kuboresha mazingira ya kujifunzia.

Katika hatua ya kuunga mkono jitihada hizo, Mhandisi Wasira ametoa kompyuta moja kwa shule hiyo, pamoja na kuahidi kusaidia kutatua changamoto nyingine zilizoainishwa. Aidha, ametoa wito kwa wazazi na jamii kwa ujumla kudumisha amani kuelekea uchaguzi mkuu ujao.