Mazingira FM
Mazingira FM
15 September 2025, 7:41 pm

Ndugu Lukas amesema azma yake kubwa ni kuiletea kata hiyo maendeleo endelevu kwa kusimamia ipasavyo miradi ya barabara, kufufua soko la Nyamakokoto
Na Catherine Msafiri,
Mgombea udiwani kupitia Chama Cha Mapinduzi (CCM) kata ya Nyamakokoto, Halmashauri ya Mji wa Bunda mkoani Mara Ndugu Lukas Daniel Marco, amezindua rasmi kampeni zake, huku akiahidi kuleta mageuzi ya maendeleo kwa wananchi wa kata hiyo hasa katika sekta ya miundombinu na huduma za kijamii.
Akizungumza mbele ya umati wa wakazi wa Nyamakokoto waliojitokeza kwa wingi, Lukas amesema azma yake kubwa ni kuiletea kata hiyo maendeleo endelevu kwa kusimamia ipasavyo miradi ya barabara, kufufua soko la Nyamakokoto, na kuhakikisha barabara zinapitika muda wote iwe kipindi cha mvua au kiangazi.

Aidha, Lukas amewaomba wagombea udiwani wenzake wa kata mbalimbali ndani ya halmashauriya mji wa Bunda kutoka chama cha CCM, kumpa ushirikiano wa karibu na nafasi katika mipango ya maendeleo, akisisitiza kuwa yeye ndiye mgombea udiwani mdogo zaidi kwa umri, lakini mwenye maono kwa vizazi vya sasa na vijavyo.
Uzinduzi huo wa kampeni ulipambwa na viongozi mbalimbali wa CCM, wakiwemo madiwani wa kata jirani pamoja na mgombea ubunge wa CCM Jimbo la Bunda Mjini, Ester Amos Bulaya, ambaye pia alipata nafasi ya kuwasalimia wananchi.