Mazingira FM
Mazingira FM
5 July 2025, 8:50 am

Matumizi ya mita za malipo ya kabla pia yatasaidia kuhimiza matumizi bora ya maji na kuongeza uwazi katika ulipaji wa huduma.
Na Adelinus Banenwa
Katika hatua ya kuimarisha huduma za usambazaji maji na kuondoa changamoto za malalamiko ya wateja kuhusu bili zisizoeleweka, Mkurugenzi wa Mamlaka ya Majisafi na Usafi wa Mazingira Bunda BUWSSA, Bi Esther Gilyoma, ametangaza kuwasili kwa mita za maji za malipo ya kabla, maarufu kama pre-paid meters.

Bi Gilyoma amesema jumla ya mita 1,000 zimepokelewa, na zitatumika kwa wateja wa zamani na wapya. Mita hizi zitasaidia kuondoa malalamiko ya kubambikiziwa bili, pamoja na kupunguza kazi ya watumishi wa mamlaka kuzunguka kusoma mita kila mwezi.
Aidha, Bi Gilyoma amewataka wananchi wote wateja wa sasa pamoja na wanaotaka kuunganishiwa huduma kufika katika ofisi za BUWSSA ili kupata maelekezo na utaratibu wa namna ya kupata mita hizo mpya.

Kwa mujibu wa mamlaka hiyo, matumizi ya mita za malipo ya kabla pia yatasaidia kuhimiza matumizi bora ya maji na kuongeza uwazi katika ulipaji wa huduma.