Mazingira FM

Anayedaiwa kuchoma moto kiganja cha mtoto wake atiwa mbaroni

23 March 2025, 12:24 pm

Wakazi wa mtaa wa Mapinduzi wakiwa kwenye ofisi ya mtaa wakimtaka mwenyekiti awapatie mtuhumiwa aliyedaiwa kumchomwa mwanae kiganja ili na wao wamchome

Mwanamke aliyedaiwa kumchoma mwanae kiganja cha mkono kwenye jiko la mkaa atiwa mbaroni wananchi wataka kumshushia kipigo.

Na Adelinus Banenwa

Ni Neema Musimu John mkazi wa  mtaa wa Mapinduzi kata ya Bunda mjini  mkoani Mara ambaye inadaiwa kumchoma moto kwenye kiganja cha mkono  mtoto wake wa kumzaa kwa sababu ya kujisaidia kwenye nguo amenusurika kipigo baada ya kutiwa mbaroni na wananchi.

Wananchi hao wakiwa wanaonekana kuwa na hasira kutokana na kitendo alichokifanya mwanamke huyo walikusanyika katika ofisi ya serikali ya mtaa wakimtaka mwenyekiti awakabidhi mwanamke huyo na wao wamchome mikono kama yeye alivyomfanya mtoto wake.

Wakazi wa mtaa wa Mapinduzi wakiwa kwenye ofisi ya mtaa wakimtaka mwenyekiti awapatie mtuhumiwa aliyedaiwa kumchomwa mwanae kiganja ili na wao wamchome

Baadhi ya mashuhua wameiambia Mazingira Fm kuwa jirani yao huyo alimchoma mtoto wake huyo siku ya tarehe 18 March 2025 kwa kosa la kujisaidia kwenye nguo na imekuwa ni kawaida yake kutoa adhabu za kupindukia  kwa mtoto huyo huku akiwatishia majirani hao kutoa taarifa

Sauti za mashuhuda

Mwenyekiti wa mtaa mapinduzi kata ya Bunda mjini Daniel Yapanda amesema mwanamke huyo wamemkamata majira ya jioni baada ya kufika nyumbani kwake akitokea jijini Mwanza anakodai alienda kufuata biashara, kisha kumfikisha ofisi za serikali za mitaa ambapo utaratibu ni kumpeleka kituo cha polisi.

Wakazi wa mtaa wa Mapinduzi wakiwa kwenye ofisi ya mtaa wakimtaka mwenyekiti awapatie mtuhumiwa aliyedaiwa kumchomwa mwanae kiganja ili na wao wamchome

Mwenyekiti Yapanda ametoa rai kwa wananchi kujenga tabia ya kutoa taarifa za matukio ya kikatili yanayofanyika katika familia ili kuepusha madhara yanayoweza kujitokeza kwa wahanga wa ukatili huo

Sauti ya Mwenyekiti mtaa Daniel Yapanda

Naye Lucia John Tabuse katibu wa jumuiya ya wazazi chama cha mapinduzi wilaya ya Bunda ambaye alimsaidia mtoto huyo kupata matibabu kwa kushirikiana na  viongozi wengine wa mtaa na kata, amewataka wazazi hasa wanawake kuwa karibu na watoto wao ili kutambua changamoto walizonazo badala ya kutoa adhabu za kikatili kwa matatizo yanayoweza kushughulikiwa kiafya.

Sauti ya Lucia John

Ikumbukwe tukio la mtoto wa umri wa miaka 5  kubainika ameunguzwa kiganja cha mkono liliibuliwa na wasamalia wema March 21, 2025 mtaa wa Mapinduzi kisha kutoa taarifa kwa viongozi ambao walichukua hatua za kumfikisha hospitali ili kupata huduma za matibabu.