Mazingira FM

Radio jamii zanolewa kumulika nafasi ya wanawake uchaguzi mkuu 2025

22 March 2025, 9:03 pm

Picha ya pamoja washiriki wa mafunzo kwa radio jamii Tanzania yaliyotolewa na TAMWA kwa kushirikiana na TADIO jijiji Dodoma

Licha ya sensa ya watu na makazi ya 2022 kuonesha idadi ya wanawake ni wengi kuliko wanaume, katika nafasi za uongozi kwa ngazi za udiwani na ubunge bado kuna idadi ndogo zaidi ya uwakilishi.

By Edward Lucas

Chama cha Wanahabari Wanawake Tanzania TAMWA kwa kushirikiana na TADIO wameendesha mafunzo kwa radio za kijamii Tanzania Bara kuandaa habari na vipindi vitakavyowawezesha wanawake kushiriki kikamilifu hasa kwa kuwania nafasi mbalimbali za uongozi katika uchaguzi mkuu wa 2025.

Akizungumzia mafunzo hayo, Meneja Mipango na Mikakati TAMWA, Sylivia Daulinge amesema mafunzo hayo yanayodhaminiwa na Mfuko wa Maendeleo ya Vyombo vya Habari Finland VIKES yamelenga elimu ya namna bora ya kuandaa vipindi vya usawa na ujumuishi wa masuala ya kijinsia kwa kuhakikisha wanawake hasa vijana na makundi maalumu yanapewa kipaumbele kuelekea uchaguzi mkuu.

Sylivia Daulinge, Meneja Mipango na Mikakati TAMWA
Sylivia Daulinge, Meneja Mipango na Mikakati TAMWA

Kwa upande wake Mkufunzi wa mafunzo hayo kutoka Radio Tadio, Hilali Alexander Ruhundwa amesema kwa kushirikiana na TAMWA wameona wanajukumu la kufanya katika jamii kwa kuwashirikisha waandishi wa habari ili kufikisha elimu kwa jamii kuwafanya wanawake washiriki kikamilifu katika uchaguzi ujao

Hilali Alexander Ruhundwa, Mkufunzi wa mafunzo kutoka Radio Tadio akieleza kuhusu malengo ya mafunzo kwa radio za jamii kuelekea uchaguzi wa 2025
Sauti ya Hilali Alexander Ruhundwa

Kwa takwimu za uchaguzi mkuu uliopita wa mwaka 2020, madiwani wanawake waliochaguliwa kwenye kata ni 260 kati ya 3,953 ambao ni sawa na asilimia 6.58 na kwa upande wa ubunge kati ya majimbo 264 wabunge wanawake waliochaguliwa kwenye majimbo ni 26 tu sawa na asilimia 9.85