Mazingira FM
Mazingira FM
16 October 2025, 4:03 pm

Wateja waombwa kuwa wavumilivu na kuelewa mazingira ya biashara ya nyama kwa sasa, huku akiahidi kuwa chama chao kitaendelea kushirikiana na wadau mbalimbali kutafuta njia ya kudhibiti mfumuko wa bei.
Na Catherine Msafiri na Teddy Thomas
Baadhi ya wafanyabiashara wa nyama katika soko la Genge la Jioni, mjini Bunda, wameelezea sababu ya kupanda kwa bei ya nyama kutoka Shilingi 10,000 hadi Shilingi 12,000 kwa kilo, wakieleza kuwa hali hiyo imesababishwa na kuongezeka kwa gharama za ununuzi wa ng’ombe katika minada mbalimbali.
Wakizungumza na Mazingira FM, wafanyabiashara hao wamesema kuwa ongezeko hilo halikwepeki kutokana na changamoto zinazoikumba sekta hiyo, ikiwemo kupanda kwa bei ya mifugo, gharama za usafirishaji, na uendeshaji wa biashara kwa ujumla.
Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Wafanyabiashara wa Nyama Bunda, Bw. Masau Magala Malima, amewahimiza wateja kuwa wavumilivu na kuelewa mazingira ya biashara kwa sasa, huku akiahidi kuwa chama chao kitaendelea kushirikiana na wadau mbalimbali kutafuta njia ya kudhibiti mfumuko wa bei.
Aidha Bw. Masau Magala Malima amebainisha kuwa kwasasa kuna upungufu wa Ng`ombe kutokana na changamoto za wafugaji kuhama hama ,uchache wa malisho na ongezeko la wanunuzi wa Ng`ombe minadani kutoka mikoa mingine.