Mazingira FM

108 mbaroni kufuatia maandamano Simiyu

21 August 2024, 10:30 pm

Mkuu wa Wilaya ya Busega, mkoani Simiyu Faiza Salim

Mkuu wa wilaya Busega mkoani Simiyu amesema waandamanaji walimrushia mawe akiwa na viongozi wengine alipofika kuwasikiliza.

Na Adelinus Banenwa

Mkuu wa Wilaya ya Busega, mkoani Simiyu Faiza Salim amesema hadi sasa watu108 wamekamatwa kufuatia maandamano yaliyofanywa na wakazi wa lamadi mapema leo 21 Aug 2024.

Mhe Faiza amesema waandamanaji wamesababisha athari kubwa kwa mali za watu na Umma ikiwemo kutaka kuchoma moto kituo cha polisi Lamadi, kuvunja vioo vya magari yaliyokuwa yakipita barabarani na baadhi ya viongozi kushambuliwa kwa kupigwa mawe akiwemo yeye mwenywe (Faiza).

Aidha Mhe DC amekili mabomu ya machozi kutumika kwa lengo la kuwazuia waandamanaji kutoleta athari zaidi na wao kama mamlaka hawawezi kukubali uharibifu kutokea.Kuhusu taarifa za waandamanaji kupoteza maisha, amesema hajapokea taarifa ya mtu yeyote kupoteza maisha isipokuwa inawezekana yapo majeraha madogo, na waliokamatwa wanasubiria kuwapeleka mahakamani.

Sambamba na hilo amesema serikali inao utaratibu wa kupokea taarifa kutoka kwa wananchi na yeye kama mkuu wa wilaya hana taarifa yoyote ya kupotea kwa watoto katika eneo hilo.

Sauti ya Mkuu wa Wilaya ya Busega, mkoani Simiyu Faiza Salim