Jamii FM
Jamii FM
12 August 2026, 16:51

Serikali imetumia zaidi ya Sh milioni 560.52 kujenga Shule ya Sekondari Chikota, Halmashauri ya Mji Nanyamba, Mtwara, huku Serikali ikiahidi kushughulikia changamoto zinazoikabili shule hiyo
Na Musa Mtepa
Serikali imewezesha ujenzi wa Shule ya Sekondari Chikota katika Halmashauri ya Mji Nanyamba mkoani Mtwara kwa gharama ya zaidi ya Sh milioni 560.52.
Kati ya fedha hizo, Sh milioni 471.4 zimetumika katika ununuzi wa vifaa vya ujenzi, huku Sh milioni 89.4 zikitumika kulipia mafundi waliotekeleza ujenzi huo.
Hayo yamesemwa leo, Agosti 12, 2026, na Mkuu wa Shule ya Sekondari Chikota, Mwalimu George Danford, wakati akitoa taarifa ya utekelezaji wa mradi huo uliojengwa katika Halmashauri ya Mji Nanyamba.

Aidha, Mwalimu Danford amesema awamu ya kwanza ya mradi huo imekamilika, huku miundombinu yote iliyopangwa katika awamu hiyo ikiwa imejengwa.
Kwa upande wake, akimwakilisha Mkuu wa Wilaya ya Mtwara, Mkuu wa Wilaya ya Tandahimba, Kanali Michael Mtenjele, amewataka wananchi, walimu na wanafunzi kutunza miundombinu ya shule hiyo ili Serikali iweze kuendelea kuboresha na kujenga miundombinu mingine katika shule hiyo na maeneo mengine nchini.

Akizungumza baada ya kuweka jiwe la msingi katika shule hiyo, Waziri wa Viwanda na Biashara, Mhe. Judith Kapinga, amesema kwa kushirikiana na Waziri wa Elimu atazifanyia kazi changamoto zinazoikabili shule hiyo, ili kuwezesha wanafunzi kupata mazingira bora ya kujifunzia na elimu yenye ubora.
Aidha, Waziri Kapinga amewataka wananchi kuendelea kushirikiana na viongozi wa Serikali, hususan pale wanapokutana na changamoto, kwa kuwafikishia taarifa na changamoto hizo kwa wakati, ili Serikali iweze kuzifanyia kazi na kuendelea kupeleka miradi mbalimbali ya maendeleo kwa wananchi na taifa kwa ujumla.
