Jamii FM
Jamii FM
12 December 2024, 13:44

Hii ilikuwa sherehe za kumpongeza Mwenyekiti wa Kijiji cha Nyengedi Bi Lukia Mnyachi baada ya kuchaguliwa na Wananchi katika nafasi hiyo.
Na Tatu Mshamu
Mwenyekiti wa Chama cha Mapinduzi (CCM) Mtwara Vijijini, Nashiri Pontiya,amewataka wenyeviti wa vijiji waliochaguliwa kupitia chama hicho kuacha kukidharau chama hicho baada ya kuchaguliwa huku akisisitiza umuhimu wa viongozi hao kusimamia vyema miradi ya maendeleo na kutumia kamati za maendeleo ili kuhakikisha manufaa kwa wananchi waliowachagua.
Ameyasema hayo December 11,2024 akiwa mgeni rasmi katika hafla iliyoandaliwa na wanachama wa CCM Kijiji cha Nyengedi kufurahia ushindi wa viongozi hao, na kuwasilisha changamoto zinazowakabili katika Kijiji hiyo, ikiwa ni ukosefu wa maji,shule,zahanati pamoja na soko.
Katika hafla hiyo, Bi.Lukia Mnyachi, Mwenyekiti wa Kijiji cha Nyengedi, ametoa shukrani kwa wananchi kwa kumuamini na kumchagua, huku akiahidi kuendelea kushirikiana nao katika maendeleo bila kujali itikadi za vyama.

Mwenyekiti wa UWT (CCM) Wilaya ya Mtwara, Bi. Mwajuma Nahembe, amewakumbusha wazazi kusimamia malezi ya watoto wa kike ili kuwaepusha na vitendo hatarishi wakati wa likizo, ili wasikose masomo.

Zuhura Farid, Mjumbe wa Halmashauri Kuu CCM Mkoa wa Mtwara, amesisitiza umoja kati ya viongozi waliochaguliwa katika Kata ya Mkunwa na kuwataka kuondoa makundi yaliyojitokeza wakati wa uchaguzi, ili kuwatumikia wananchi kwa umoja.
