Jamii FM

Kamati ya Amani Mkoa wa Mtwara, yamuombea Dua Rais Samia

21 March 2023, 11:00 am

Wanakamati ya Amani wakiomba Dua maalumu Mkoani Mtwara. Picha na Musa Mtepa

utaratibu wa kumyombea tua na kumpongeza kiongozi wa nchi kwa miaka miwili ya Uongozi umekuwa ukifanyika kila mahali nchini Tanzania na Mkoani Mtwara wamemuombea Dua Mh. Rais Samia kwa Kazi nzuri anayoifanya

Na Musa Mtepa

Baraza la kiislamu Tanzania (BAKWATA) kwa kushirikiana na kamati ya Amani na Maridhiano mkoa wa Mtwara imefanya Dua ya kumpongeza Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dr Samia Suluhu Hassani kwa kutimiza miaka miwili tangu aingie Madarakani na kazi nzuri anayoendelea kuifanya ya kuwaletea Maendeleo Watanzania.

Barabara ya Uchumi ya Mtwara,Tandahimba, Newala – Masasi inatarajia kuanza ujenzi huo mwezi wa sita mwaka huu 2023

Akitoa taarifa kwa Mgeni rasmi katibu wa kamati ya amani na maridhiano mkoa wa Mtwara Askofu wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT), Dayosisi ya Kusini Mashariki, Lucas Mbedule amesema kuwa katika kuadhimisha miaka miwili ya Rais Samia wamedhamiria kumuombea Dua na kumpongeza kwa kazi nzuri anayendelea kuifanya kwa kuendelea kuijenga Tanzania katika miundombinu mbalimbali.

Askofu wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT), Dayosisi ya Kusini Mashariki, Lucas Mbedule. Picha na Musa Mtepa

Aidha askofu Mbedule amesema kuwa katika kipindi cha miaka miwili amefanikiwa kutengeneza na kuimarisha miundombinu mbalimbali ya kimaendeleo ikiwemo ujenzi wa Zahanati , Vituo vya Afya na Hospitali za Rufaa na katika Sekta ya usafirishaji huku akimpongeza Mh Rais kwa juhudi za kujenga amani na Demokrasia hasa kwa kitendo cha kuchukua muda wake wa kukaa na vyama vyote na kuridhia mahitaji ya viongozi wa vyama vya siasa ikiwa ni hatua mzuri na ya mfano kwa nchi nyingine.

Kwa upande wake mgeni rasmi ambae pia ni Mwenyekiti wa Chama cha mapinduzi mkoa wa Mtwara kwa niaba ya Mkuu wa mkoa Saidi Musa Nyengedi amesema kuwa viongozi wa Dini na kamati ya amani na maridhiano imefanya kitu kikubwa cha kumpongeza na kumfanyia Dua Rais Samia kwa kazi kubwa anayoifanya ya kuleta amani na maendeleo katika kipindi cha miaka miwili nchini.Mh Nyengedi amesema kuwa Rais kwa kipindi cha miaka miwili amefanikiwa kugusa kila eneo katika mkoa wa Mtwara kama vile ujenzi wa Madarasa kwa shule za msingi na sekondari, vituo vya Afya, ujenzi wa Miradi ya maji pamoja na Barabara.

Akiigusia Barabara ya Uchumi ya Mtwara,Tandahimba, Newala – Masasi Mh Nyengedi amesema kuwa katika kipindi hiki kifupi Rais Dr Samia ametoa Bilioni 268 kwa ujenzi wa Barabara hiyo huku matarajio ya kuanza ujenzi huo ni kuanzia mwezi wa sita mwaka huu hivyo kilichofanywa na BAKWATA pamoja na kamati ya Amani na Maridhiano jambo la kiungwana na la kupongezwa.

Naye Shekhe mkuu wa mkoa wa Mtwara Nurudin Abdala Mangochi amesema kuwa kiongozi mkuu wa serikali anatakiwa kutawala vizuri pamoja na anaowatawala, ili maendeleo yapatikane kutokana na huo utawala na ndio sababu iliyowapelekea kuandaa Dua na pongezi kwa Rais Samia kutokana na mazuri anayoendelea kuyafanya.