Jamii FM

Usambazaji wa pembejeo za korosho 2026/2027 waanza rasmi nchini

28 April 2026, 11:19

Upakiaji wa pembejeo ukiwa unaendelea kutoka kwenya ghala kuelekea vyama vikuu vya ushirika ikiwa tayari maandalizi ya upuliziaji kwa msimu wa korosho 2026/2027 (Picha na Musa Mtepa)

Bodi ya Korosho Tanzania yaanza kusambaza zaidi ya tani 50,000 za pembejeo, ikiwemo salfa na viuatilifu, huku wakulima wakihimizwa kutumia kwa usahihi kuongeza uzalishaji wa korosho nchini.

Na Musa Mtepa

Zoezi la usambazaji wa pembejeo za zao la korosho limeanza rasmi kwa msimu wa kilimo wa 2026/2027, huku matarajio yakionyesha zaidi ya tani 50,000 za pembejeo kusambazwa katika mikoa yote inayolima korosho nchini.

Akizungumza kwa niaba ya Mkurugenzi Mkuu wa Bodi ya Korosho Tanzania (CBT), Meneja wa Mipango ya Kilimo, Juma Yusufu, amesema bodi imejipanga kusambaza tani 30,000 za salfa ya unga pamoja na lita milioni 1.5 za viuatilifu vya maji  na kuongeza kuwa mfumo wa kidigitali utaendelea kutumika katika kurahisisha usambazaji na ugawaji wa pembejeo hizo kwa wakulima.

Sauti ya Juma Yusufu – Meneja wa Mipango ya Kilimo, CBT

Aidha, Juma Yusufu amesema CBT kwa kushirikiana na wadau mbalimbali imejipanga kutoa mafunzo kwa wakulima kuhusu matumizi sahihi na salama ya pembejeo hizo, hatua inayolenga kuongeza tija na uzalishaji wa korosho nchini.

Sauti ya Juma Yusufu – Meneja wa Mipango ya Kilimo, CBT

Kwa upande wake, Kaimu Meneja wa Ushirika wa mradi wa pamoja wa vyama vikuu vya korosho nchini (KCJE), Mabruki Mpangula, amesema tayari wana tani 16,000 za salfa zilizobaki kutoka msimu uliopita. Ameongeza kuwa wameingia mkataba na wazabuni kwa ajili ya kuagiza tani 35,000 zaidi, na hivyo kufanya jumla ya matarajio kufikia tani 51,000 za salfa kwa msimu mzima wa 2026/2027.

Sauti ya Mabruki Mpangula – Kaimu Meneja KCJE

Naye Afisa Kilimo kutoka Chama Kikuu cha Ushirika MAMCU, Salumu Faki, amewataka wakulima kuwa tayari kupokea pembejeo hizo na kuanza matumizi ya viuatilifu vya maji kwa wakati ili kudhibiti wadudu waharibifu wa mikorosho.

Sauti ya Salumu Faki – Afisa Kilimo, MAMCU