Jamii FM
Jamii FM
27 April 2026, 23:38

Wananchi wa Kitaya, Mtwara, walalamikia uharibifu wa mazao unaosababishwa na wanyama pori, wakiiomba serikali kuchukua hatua huku viongozi wakieleza jitihada na tahadhari zinazopaswa kuchukuliwa
Na Musa Mtepa
Wananchi wa Kijiji cha Kitaya kilichopo katika Kata ya Kitaya, Halmashauri ya Mji Nanyamba mkoani Mtwara, wameiomba serikali kuangalia kwa jicho la tatu changamoto ya wanyama wanaoharibu mazao yao mashambani.
Wakizungumza katika mkutano wa kijiji uliofanyika Aprili 24, 2026 katika viwanja vya ofisi za kijiji hicho, wananchi wamesema changamoto ya wanyama wanaoshambulia mazao imekuwa sugu kwa wakulima, licha ya kuiwasilisha mara kadhaa katika halmashauri bila mafanikio yoyote.
Aidha, wakulima hao wamesema wanyama wanaosumbua mashamba yao ni pamoja na ngedele, kima, boko, ngiri na tembo, ambao wamekuwa wakivuka kutoka upande wa Msumbiji na kuingia kwenye mashamba ya wakulima wa vijiji vya Tanzania.
Akizungumzia changamoto hiyo, Mheshimiwa Diwani wa Kata ya Kitaya, Abdalah Chalamanda, amesema kuwa alipoingia madarakani alikuta tatizo hilo na kulifikisha katika ngazi ya halmashauri kupitia ofisi ya maliasili, lakini hadi sasa hatua stahiki hazijachukuliwa kuwasaidia wakulima hao.
Kwa upande wake, Afisa wa Wanyamapori Mkoa wa Mtwara, Keneth Sanga, ameelezea utaratibu wa kufanya tathmini ya madhara yanayosababishwa na wanyama pori. Pia ametoa wito kwa wakulima kuzingatia taratibu za kulima karibu na maeneo ya hifadhi za wanyamapori na kuchukua tahadhari za kujikinga na hatari za wanyama hao katika maeneo yao.