Jamii FM
Jamii FM
16 June 2026, 10:32

Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora imetoa mafunzo kwa wavuvi wadogo Msangamkuu kuhusu haki za binadamu, matumizi sahihi ya rasilimali za bahari na namna ya kushughulikia matukio ya uvunjifu wa haki ili kupunguza migogoro
Na Musa Mtepa
Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora imetoa mafunzo kuhusu haki za binadamu kwa wavuvi wadogo wa Kijiji cha Msangamkuu kwa lengo la kuwajengea uelewa kuhusu haki hizo na namna ya kuzifikia pale zinapovunjwa.
Akizungumza Juni 15, 2026, wakati wa mafunzo hayo, Katibu Mtendaji wa Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora, Patience Ntwina, amesema wamebaini kuwa utekelezaji na usimamizi wa matumizi ya rasilimali za bahari umekuwa na changamoto mbalimbali, hivyo kuna umuhimu wa kuhakikisha kila mtu ananufaika na rasilimali hizo bila kuingiliana au kuathiriana kati ya wavuvi na wakulima wa mwani.

Aidha, Ntwina amesema kuwa si Msangamkuu pekee itakayonufaika na mafunzo hayo, bali pia maeneo mengine ya ukanda wa pwani mkoani Mtwara yatapatiwa elimu hiyo. Amesisitiza umuhimu wa kuzingatia mafunzo hayo ili kila mmoja aweze kunufaika na rasilimali za bahari bila kuvunja haki za binadamu za wengine.

Kwa upande wake, Katibu wa BMU wa Kijiji cha Sinde, Faruck Hilari, amesema kuwa moja ya sababu zinazochangia migogoro kati ya wadau wa matumizi ya rasilimali za bahari ni ukosefu wa uelewa wa kutosha katika usimamizi wa sheria na kanuni. Amesema mafunzo hayo, yaliyowakutanisha wadau mbalimbali, yatasaidia kupunguza migogoro hiyo, huku akiiomba Serikali na wadau wengine kuendelea kutoa elimu kuhusu matumizi sahihi ya rasilimali za bahari.

Nao baadhi ya washiriki wa mafunzo hayo wamesema elimu waliyoipata itawasaidia kukabiliana na changamoto wanazokutana nazo katika shughuli za matumizi ya rasilimali za bahari, pamoja na kuwajengea uwezo wa kutambua na kuchukua hatua wanapokumbana na vitendo vya uvunjifu wa haki za binadamu.
