Jamii FM
Jamii FM
26 June 2026, 18:36

Wakulima na wavuvi wa Mbuyuni/Mwambo, Kijiji cha Kilambo mkoani Mtwara, wameiomba Serikali kujenga daraja la kudumu eneo la Mtando ili kurahisisha usafirishaji wa mazao, kuongeza usalama wa watumiaji na kuimarisha shughuli za kiuchumi
Na Musa Mtepa
Wakulima na wavuvi wanaofanya shughuli zao katika eneo la Mbuyuni/Mwambo, Kijiji cha Kilambo, Halmashauri ya Wilaya ya Mtwara mkoani Mtwara, wameiomba Serikali kujenga daraja katika eneo la Mtando ili kurahisisha usafirishaji wa mazao na shughuli nyingine za kiuchumi.
Wakizungumza na Jamii FM Redio, wananchi hao wamesema eneo hilo ni njia muhimu ya kupitisha mazao mbalimbali yanayochangia mapato ya kijiji na Halmashauri kupitia ushuru, hivyo wanaamini ujenzi wa daraja la kudumu utasaidia kuongeza ufanisi wa shughuli za uzalishaji na biashara.

Akizungumzia hali ya daraja linalotumika kwa sasa, mkazi na mkulima wa Kijiji cha Kilambo, Mohamedi Dadi Mkoba, amesema daraja hilo limejengwa kwa kutumia miti ambayo huathirika kwa kuoza kadri muda unavyopita, hali inayoweza kuhatarisha usalama wa watumiaji wake siku zijazo.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Kijiji cha Kilambo, Mohamed Ali, amesema suala la daraja hilo liliwahi kujadiliwa katika mikutano ya kijiji na hata kuwasilishwa kwa wataalamu waliofika eneo husika kufanya tathmini na vipimo.
Amesema baada ya tathmini hiyo, wataalamu walieleza kuwa haikuwezekana kutekeleza ujenzi wa daraja hilo kwa kipindi hicho, jambo ambalo limeendelea kuwaacha wananchi wakisubiri utekelezaji wa mradi huo muhimu.