Jamii FM

Mtwara yawakutanisha wataalamu wa Korosho barani Afrika

2 June 2026, 11:21

Baadhi ya washiriki wa mafunzo wakifuatilia kwa umakini ufunguzi wa mkuu wa mkoa wa Mtwara Kanali Dolnad Msengi yaliyofanyika jana June 1 ,2026 katika ukumbi wa mikutano wa Benki kuu BOT tawi la Mtwara.

Mtwara imekuwa mwenyeji wa mafunzo ya kimataifa ya korosho yaliyowakutanisha washiriki kutoka zaidi ya nchi 11 za Afrika kujadili mbinu za kuongeza uzalishaji, thamani na masoko ya zao la korosho kwa manufaa ya wakulima na wadau wa sekta hiyo

Na Musa Mtepa

Mkoa wa Mtwara umekuwa mwenyeji wa mafunzo ya kimataifa kuhusu zao la korosho yenye lengo la kubadilishana uzoefu, maarifa na kuimarisha mikakati ya kuongeza thamani ya zao hilo katika nchi mbalimbali za Afrika.

Mafunzo hayo, ambayo hufanyika kila mwaka katika maeneo yanayolima korosho, yanafanyika kwa mara ya pili mfululizo mkoani Mtwara na yamewakutanisha washiriki kutoka zaidi ya nchi 11 za Afrika kwa lengo la kuendeleza sekta ya korosho barani humo.

Akizungumza wakati wa ufunguzi wa mafunzo hayo, Mkuu wa Mkoa wa Mtwara, Kanal Donald Msengi, amesema lengo kuu la mafunzo hayo ni kubadilishana uzoefu na maarifa yatakayosaidia kuongeza thamani ya zao la korosho na kuboresha maisha ya wakulima kupitia ongezeko la uzalishaji na mapato.

Sauti ya Kanal Donald Msengi, Mkuu wa Mkoa wa Mtwara

Aidha, Kanal Msengi amesema kufanyika kwa mafunzo hayo mkoani Mtwara ni fursa muhimu kwa maendeleo ya kiuchumi ya mkoa huo, kwani wageni wanaoshiriki hutumia huduma mbalimbali za kijamii na kiuchumi zikiwemo malazi, chakula na usafiri, jambo linalochochea biashara za ndani na kuitangaza Mtwara katika ngazi ya kimataifa.

Sauti ya Kanal Donald Msengi, Mkuu wa Mkoa wa Mtwara
Mkuu wa mkoa wa Mtwara Kanal Dolnad Msengi akifungua mafunzo

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mkuu wa Bodi ya Korosho Tanzania (CBT), Francis Alfred, amesema mafunzo hayo yaliyoandaliwa na Jukwaa la Korosho Afrika (African Cashew Alliance) yamefanyika Mtwara kutokana na mafanikio makubwa ambayo Tanzania imepata katika sekta ya korosho, hususan katika huduma za ugani na tafiti za kilimo.

Amesema Tanzania imekuwa mfano wa kuigwa kwa nchi nyingine kutokana na mfumo wake wa kuwapeleka vijana wahitimu kutoka vyuoni kuwahudumia wakulima katika maeneo ya vijijini, pamoja na mchango wa tafiti zinazofanywa na Taasisi ya Utafiti wa Kilimo Tanzania (TARI) Naliendele katika kuboresha uzalishaji wa korosho.

Sauti ya Francis Alfred, Mkurugenzi Mkuu wa CBT
Mkurugenzi mkuu wa Bodi ya Korosho CBT Ndug Frances Alfred akizungumza washiriki wa mafunzo hayo yaliyofanyika june 1 ,2026 mjini Mtwara.

Naye meneja wa maendeleo ya rasilimali watu Jukwaa la Korosho Afrika( African Cashew Alliance), Reine Dehode, amesema mafunzo hayo yanalenga kuimarisha mnyororo mzima wa thamani wa zao la korosho kuanzia uzalishaji shambani, uchakataji hadi upatikanaji wa masoko.

Amebainisha kuwa washiriki kutoka nchi mbalimbali za Afrika wanatumia jukwaa hilo kujifunza mbinu bora za uzalishaji, uchakataji na masoko ya korosho ili kuongeza tija, ubora wa bidhaa na mapato kwa wadau wa sekta hiyo.

Sauti ya Reine Dehode, Meneja wa Maendeleo ya Rasilimali Watu, Jukwaa la Korosho Afrika

Baadhi ya washiriki wa mafunzo hayo wamesema yamewapa fursa ya kujifunza teknolojia mpya za uzalishaji wa miche bora ya korosho, mbinu za kuongeza thamani ya zao hilo pamoja na njia za kuboresha masoko, hatua ambazo zinaweza kuongeza faida kwa wakulima na wadau wengine wa sekta ya korosho.

Sauti za washiriki wa mafunzo hayo
Washiriki wa mafunzo wakifuatilia kinacholezwa na wataalamu kwenye mafunzo