Baraka FM

Moravian Mbarali kupaua ofisi za kanisa kwa debe la mpunga kwa kila mkristo

20 April 2026, 22:21

Hii ni kamati ya ya hamasa ya upauaji wa ofisi za kanisa la Moravian wilaya ya Mbarali wakiwa na mgeni rasmi wa tatu (kushoto waliokaa)picha na Hobokela Lwinga

Kanisa la Moravian Tanzania Jimbo la kusini magharibi limeendelea kuboresha ofisi zake ikiwa ni kuweka mazingira Rafiki ya ufanyaji kazi ya Mungu.

Na Hobokela Lwinga

Wilaya ya Mbarali  Kanisa la Moravian Tanzania Jimbo la Kusini Magharibi, imezindua rasmi harambee ya ujenzi kwa ajili ya upauaji wa ofisi za wilaya hiyo.‎‎

Ibada ya uzinduzi wa harambee hiyo ilifanyika mwishoni mwa wiki katika Kanisa la Moravian Ushirika wa Igurusi, na kuhudhuriwa na viongozi mbalimbali wa kanisa pamoja na serikali. Katika harambee hiyo,kila Mkristo ndani ya wilaya ya Mbarali anahimizwa kuchangia debe moja la mpunga ili kufanikisha zoezi hilo.

‎‎Akifungua ibada hiyo kwa niaba ya Askofu wa kanisa la Moravian Jimbo la kusini magharibi Robert Pangani, Mwenyekiti wa Kanisa la Moravian Wilaya ya Mbarali, Mchungaji Paul Mwampamba,aliwataka waumini kutambua wajibu wao wa kutoa sadaka kwa ajili ya ujenzi, ili kuendeleza kazi ya Mungu katika wilaya hiyo.

Mwenyekiti wa Kanisa la Moravian Wilaya ya Mbarali, Mchungaji Paul Mwampamba akiwa amebeba debe la mpunga kwa kiashirio cha uzinduzi (picha na Hobokela Lwinga)

‎‎Aidha, Mchungaji Mwampamba amesisitiza kuwa ujenzi wa ofisi hizo hautakuwa na manufaa kwa waumini wa Moravian pekee, bali utahudumia jamii nzima ya Mbarali.

‎‎Katika hatua nyingine, ametoa shukrani kwa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa ushirikiano unaoendelea kuitoa kwa kanisa katika utekelezaji wa mipango mbalimbali ya maendeleo.‎‎

Baadhi ya waumini kanisa la Moravian wilaya ya Mbarali wakiwa ndani ya ibada (picha na Hobokela Lwinga)

Akisoma risala kwa mgeni rasmi, Katibu wa wilaya ya Mbarali Mchungaji Laida Msangawale ameeleza kuwa hadi sasa ujenzi huo umefikia hatua ya lenta, ukiwa umegharimu kiasi cha shilingi milioni 50. Aliongeza kuwa wilaya inalenga kukusanya jumla ya shilingi milioni 100 ifikapo tarehe 7 Juni, 2026.

Katibu wa wilaya ya Mbarali Mchungaji Laida Msangawale (picha na Hobokela Lwinga)

‎‎Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Kamati ya Hamasa ya Ujenzi amewahimiza waumini kutotegemea wengine katika zoezi hilo, bali kila mmoja achukue jukumu la kuchangia ili kujenga historia ya kukumbukwa katika kulijenga kanisa la Mungu.

Mwenyekiti wa Kamati ya Hamasa ya Ujenzi(picha na Hobokela Lwinga)

‎‎Katika hafla hiyo, mgeni rasmi ambaye ni Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Mbarali, Mhe. Twalibu Lubandamo, alichangia shilingi milioni 10 kuunga mkono juhudi za ujenzi huo huku akisema taasisi za dini zimekuwa na mchango mkubwa wa kuhamasisha Amani nchini.

Mgeni rasmi ambaye ni Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Mbarali, Mhe. Twalibu Lubandamo(kulia)-picha na Hobokela Lwinga

‎‎Harambee hiyo inaendeshwa chini ya kauli mbiu isemayo:‎“Debe langu moja la mpunga litapaua jengo letu.”‎