Baraka FM

Mwizi wa simu ahukumiwa miaka 30 jela

21 March 2024, 18:00

Sheria ni msumeno unaokatakata kuwili na sheria ni mwongozo unaotumika kuongoza mambo fulani iwe kwenye kikundi au nchi fulani, taifa la Tanzania ni miongozni mwa mataifa yanayoongozwa na sheria kupitia katiba ya nchi .

Na Mwandishi wetu

Mahakama ya Wilaya ya Momba, mkoani Songwe tarehe 15 Machi, 2024 imemhukumu mshtakiwa Rashid Mdete (24) mkazi wa Posta Njombe kutumikia adhabu ya kifungo cha miaka 30 jela kwa kosa la unyang’anyi wa kutumia silaha.

Mshtakiwa alitenda kosa hilo mnamo tarehe 16 Februari, 2023 majira ya saa 01:30 usiku huko katika msitu wa Nyimbili barabara ya Mlowo-Kamsamba kata ya Mkomba mkoani Songwe ambapo aliiba simu 10 za aina tofautitofauti zenye thamani ya shilingi 11,400,000 za Kitanzania pamoja na fedha taslimu 750,000 za Kitanzania mali za walalamikaji.

Mshtakiwa kabla ya kuiba fedha na simu alitumia nguvu kwa kuziba njia hiyo kwa kuweka vizuizi vya mawe na magogo kisha kuwavamia kwa kumwekea walalamikaji panga shingoni na kuwatishia bunduki jambo ambalo ni kosa kinyume na kifungu namba 287A cha Sheria ya Kanuni ya adhabu Sura ya 16 ya namba 2022.

Akisoma maelezo ya hukumu ya kesi namba 34 ya mwaka 2023, Hakimu Mkazi wa Wilaya ya Momba Mheshimiwa Timothy Lyon amesema mahakama imejiridhisha na ushahidi uliotolewa na mashahidi 14 wa upande wa mashtaka ambao hauna chembe ya shaka na kumtia hatiani mtuhumiwa huyo.