Baraka FM

Askari polisi waliotimiza miaka 30 jeshini watoa msaada wa kumuwekea umeme mzee mkisi

28 December 2023, 18:17

Na mwandisi wetu,Songwe

Baadhi ya askari Polisi waliotimiza miaka 30 katika utumishi wao ndani ya Jeshi la Polisi Depo la Mwaka 1993,  wamemtembelea Kamishna Msaidizi Mwandamizi wa Polisi SACP Mkisi ambaye aliwahi kuwa Mkuu wa Shule ya Polisi Moshi (CCP) kwa sasa amestaafu utumishi kwa mujibu wa sheria kwa ajili ya kumsalimia na kufanya tafrija baada ya kumuwekea umeme nyumbani kwake.

Akiongea kwa niaba ya Wadepo hao Kamanda wa Polisi mkoa wa Songwe Kamishna Msaidizi wa Polisi ACP Theopista Mallya alisema umeme huo umetokana na fedha ambazo wamechanga ili kuweza kumsaidia Mzee Mkisi kupata umeme nyumbani kwake.

“Tumemua kufanya hivi baada ya mimi nilipokuja kumtembelea mzee Mkisi Disemba 04, 2023 na akaniambia kuwa, nyumbani kwake hakuna umeme ndipo nilipowaambia wenzangu na kuweza kulitatua swala hili, tumefanya hivi kwa nia ya kumshukuru Mungu kwa afya na  uzima katika kipindi chote cha miaka 30 ya utendaji wa kazi ndani ya Jeshi la Polisi kwa maana kuna baadhi ya wenzetu ambao tulitamani kuwa nao lakini hatupo nao kwa sababu mbalimbali”. Alisema Kamanda Mallya.

Kwa upande wake Mzee Mkisi aliwashukuru kwa dhati Depo la Mwaka 1993 kwa kitendo chao cha kumuwezesha kuwekewa umeme nyumbani kwake na aliwaomba waendelee kuwa na moyo huo wakuwasaidia wahitaji na wasiishie kwake tu bali hata kwa watu wengine.