Baraka FM

Mafanikio mapya hospitali ya rufaa Kanda ya Mbeya

29 January 2024, 18:39

Na Ezekiel Kamanga

Hospitali ya Rufaa ya Kanda ya Mbeya jana imefanya hafla fupi ya kuwakaribisha madaktari bingwa na wauguzi ambao walikuwa masomoni.

Hafla hiyo iliandaliwa katika bustani ya Mbeya Peak na kuhudhuriwa na viongozi wa hospitali na wafanyakazi wa hospitali.

Katika hafla hiyo, madaktari bingwa walipewa fursa ya kuzungumza na kuelezea uzoefu wao katika masomo yao na jinsi walivyopata maarifa na ujuzi mpya. Walishirikisha pia changamoto walizokutana nazo na jinsi walivyoweza kuzishinda.

Akizungumza katika hafla hiyo, Mkurugenzi Mtendaji wa Hospitali ya Rufaa ya Kanda ya Mbeya, Dkt. Godlove Mbwanji, aliwapongeza na kuwashukuru madaktari na wauguzi waliokuwa masomoni.

Pia, alielezea furaha yake kuona sehemu kubwa ya wafanyakazi waliotoka masomoni ni wanafunzi bora “best students” katika vyuo vyao.Hafla hiyo ilikuwa fursa nzuri ya kuimarisha ushirikiano na kuchochea maendeleo ya hospitali.

Madaktari na wauguzi hao walitambuliwa kama wataalamu wenye ujuzi mkubwa ambao watachangia katika kuboresha huduma kwa wagonjwa wa Hospitali ya Rufaa ya Kanda ya Mbeya.