Baraka FM

DC Malisa: Wahujumu uchumi mbolea ya ruzuku kukiona Mbeya

18 January 2024, 20:27

Na Hobokela Lwinga

Mkuu wa wilaya ya Mbeya Mkoani Mbeya Mh.Beno Malisa ametoa onyo kali kwa wakulima,mawakala wa mbolea na wanaoshiriki kuhujumu mpango wa mbolea ya ruzuku iliyotolewa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt Samia Suluhu Hassan kwa lengo na kumkomboa mkulima.

Akizungumza kwenye kikao cha pembejeo wilayani Mbeya kilichowashirikisha mawakala wa mbolea ya ruzuku ,maafisa kilimo na wakaguzi wa mbolea Mh.Malisa amesema wakulima wamekuwa chanzo kikubwa cha kuwasaidia mawakala kufanya udanganyifu kwenye zoezi hili la mbolea ya Ruzuku.

Mkuu huyo wa Wilaya ameongeza kuwa serikali itawachukulia hatua kali wakulima wanaokubali taarifa zao zitumike katika kufanya udanganyifu kwa kuwanufaisha baadhi ya mawakala wa mbolea ya ruzuku wasio waaminifu kwani kufanya hivyo ni sawa na kuhujumu zoezi la mbolea hiyo lenye malengo chanya kwa wakulima nchini.

Wilayani wakulima 135,635 wamejitokeza kujisajili na kuhuwisha taarifa zao katika mfumo wa mbolea ya ruzuku ambapo Mbeya Vijijini wakulima wakulima 99,312 kati yao wanawake 48,657 na Wanaume 50,604 kwa upande wa Halmashauri ya Jiji la Mbeya jumla ya wakulima 36,503 Wanawake wakiwa 21,088 na Wanaume 15,404.

Mmoja wa bwana shamba kutoka kampuni ya HAKIKA ambao ni wasambazaji na wauzaji wa Mbolea ya ruzuku ,Bwa.Hamisi Kilanga ameiomba Serikali kutoa elimu ya kutosha kwenye mfumo wa sasa umaotumika kwasababu mara nyingi umejitokeza usumbufu pale ujumbe wa mfumo unaposhindwa kurudisha ujumbe ili mteja aweze kupewa mbolea.

Kwa upande mwingine Bw.Kilanga ameiomba Serikali kuweka bei kamili ya mbolea kwa vile senti zilizopo kwenye bei za sasa zinawasumbua kwenye chenji pale ambapo mkulima anadai cheni yake hivyo kama elfu 74 au 75 iwe bila senti.

Aidha Mh.Malisa amewataka wakulima kutumia vizuri fursa hii ya kutumia mbolea ya ruzuku inayotolewa na serikali ya awamu ya sita chini ya Mh.Rais Dkt Samia Suluhu Hassan yenye malengo ya kuongezaji tija katika kilimo sambamba na kumuongezea kipato mkulima.

Kikao kijacho cha pembejeo wilayani Mbeya kinataraji kukutana tena mnamo februari 18 mwaka 2024.