Baraka FM

Bodaboda zingatie Sheria za usalama barabarani

9 January 2024, 18:38

Na mwandishi wetu,Songwe

Madereva wa Pikipiki maarufu kama Bodaboda wa Wilaya ya Momba Mkoa wa Songwe wametakiwa kufuata sheria za usalama barabarani na kuzingatia matumizi sahihi ya barabarani ikiwa ni pamoja na kuacha kujihusisha na usafirishaji wa bidhaa za magendo ili kujiepusha na mkono wa sheria.

Rai hiyo imetolewa na Mkaguzi Kata ya Mwakakati Mkaguzi Msaidizi wa Polisi Philipo Robert wakati akitoa elimu ya usalama barabarani kwa maafisa usafirishaji hao.

Aidha, Mkaguzi Philipo amewasihi madereva hao kuwa makini na abiria wanaowabeba nyakati za usiku na pindi wawatiliapo shaka watoe taarifa kwa Jeshi la Polisi ili taarifa hizo ziweze kushughulikiwa kwa haraka.

Sambamba na hayo, Mkaguzi Philipo amewaelimisha namna bora na umuhimu wa kutoa taarifa za wahalifu na uhalifu ili kudhibiti vitendo vya uhalifu kwenye jamii.