Baraka FM

Elimu kwa mlipa kodi,wananchi wafurahia

19 December 2023, 19:58

Na mwandishi wetu

Halmashauri ya wilaya ya rungwe  imeanza zoezi la kutoa elimu kwa mlipa kodi lengo likiwa ni kuwajengea uelewa wananchi faida ya kutoa kodi kwa maendeleo ya taifa letu.

Katika soko la ndizi mabonde  tukuyu mjini leo, wananchi wamepata nafasi ya kutoa changamoto mbalimbali wanazokabiliana nazo ikiwemo uelewa mdogo wa namna kodi za maendeleo zinavyochochea utekelezaji wa miradi mbalimbali ya maendeleo ambapo pamoja na mambo mengine watalamu wa kodi na mapato wamezitolea majibu na suluhu ya changamoto mbalimbali.

Wameeleza kuwa ujenzi wa vyumba vya madarasa, zahanati, vituo vya afya pamoja na stendi ya daladala tukuyu mjini ni zao la kodi za wananchi wanaotoa bila shuruti yoyote.

Aidha  upanuzi wa soko la kiwira , tandale tukuyu mjini, mikopo kwa wanawake, vijana na watu wenye ulemavu  pamoja na ununuzi wa  gari jipya la kuzoa taka ni matunda ya walipa kodi kutoka wilaya ya rungwe.

Zoezi  la elimu linaendelea katika masoko yote, stendi za mabasi, bodaboda,  na maeneo mengine mengi.

Mpaka kufikia mwenzi novemba  mwaka huu 2023 , halmashauri ya wilaya ya rungwe imekusanya mapato yake kwa asilimia 62% ya mwaka wa fedha 2023/24