Baraka FM

Ruwasa Mbeya watoa msaada kwa waathirika wa maporomoko Kawetere

19 April 2024, 17:40

Baadhi ya Watumishi wa Idara ya Maji safi na usafi wa mazingira(MBEYAUWSA) (picha na Ezekiel Kamanga)

Maporomoko mlima Kawetere yalitokea April 14,2024 majira ya saa tatu asubuhi na kusababisha nyumba zaidi ya ishirini kufukiwa na udongo ikiwemo shule ya mchepuo wa kiingereza ya Generation.

Na Ezekiel Kamanga

Bodi ya Mamlaka ya Maji Safi na Usafi wa Mazingira Mbeya ( MBEYAUWSA) ikiongozwa na Mwenyekiti wake Bi Edina Mwaigomole imetembelea Kambi ya waathirika wa maporomoko mlima Kawetere iliyopo shule ya msingi Tambuka reli Kata ya Itezi Jijini Mbeya na kutoa msaada wa vyakula kwa lengo la kuwatia moyo.Mkurugenzi Mtendaji wa Mamlaka ya Maji Safi na Usafi wa Mazingira Mbeya CPA Gilbert Kayange amesema amesema ujio wao ni ishara ya upendo na kuwatia moyo waathirika wa tukio hilo huku akiwapongeza Viongozi mbalimbali ambao wamelichukua suala hilo kwa uzito mkubwa.

CPA Gilbert Kayange amesema vyakula vilivyotolewa ni pamoja na kilo mia nne za mchele,kilo mia mia mbili za maharage na mafuta lita hamsini.Kwa niaba ya Bodi Mwenyekiti wa wake Bi Edina Mwaigomole amesema kilichotolewa ni kile ambacho kinatokana na makusanyo ya ankara za maji hivyo wanelazimika kusitisha mambo mengine ili kutoa faraja.Akipokea msaada huo Diwani wa Kata ya Itezi Jijini Mbeya Sambwee Shitambala amemshukuru kupokea msaada huo zaidi akiwaomba wadau kuchangia vyakula kutokana na uhitaji mkubwa wanapofanya maandalizi ya kuivunja kambi hiyo.”Tunaomba zaidi viletwe vyakula ili waathirika waweze kupatiwa wanapokwenda maeneo mengine”alisema Shitambala.